Mkurugenzi wa Ubora na Uhakiki wa Wizara ya Afya, maendeleo ya jamii, jinsia Wazee na Watoto Dr. Mohamed Mohamed akifungua kongamano la kimataifa la madaktari bingwa wa upasuaji wa Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu.
Mkurugenzi wa ubora na uhakiki wa Wizara ya Afya,Maendeleo ya jamii, Jinsia ,Wazee na
Watoto Dkt Mohamed Mohamed leo tarehe 5/11/2018 amefungua kongamano la tano kimataifa
la mafunzo ya madaktari bingwa wa upasuaji wa Ubongo, Mgongo na Mishipa ya fahamu katika
ukumbi mpya wa Mikutano MOI ambapo mafunzo yanafanyika kwa siku tano, siku mbili za
nadharia na siku tatu za mafunzo ya vitendo ambayo itahusisha upasuaji.
Dkt Mohamed amesema kongamano hili la tano limehudhuriwa na zaidi ya madaktari 100
kutoka nchi za Tanzania, Kenya, Ethiopia, Malawi, Namibia na nchi nyingine za Afrika, ulaya,
na marekani ambapo mafunzo yatatolewa na Madaktari bingwa 8 wazalendo kutoka MOI na
wengine 15 kutoka Marekani na Ulaya.
Mwenyekiti wa Bodi ya wadhamini ya MOI Prof Charles Mkonyi akizungumza katika kongamano la kimataifa la madaktari bingwa wa upasuaji wa Ubongo, Mgongo na Mishipa ya fahamu.
Mkurugenzi Mtendaji wa MOI Dkt Respicious Boniface amesema mafunzo haya yameratibiwa
na Taasisi ya MOI kwa kushirikiana na Chuo kikuu cha Weil Cornel cha New York Marekani
ambapo hii ni mara ya tano kufanyika hapa Tanzania (MOI).
“Mafunzo ya mwaka huu yatakuwa ya kipekee zaidi kwani wataalamu wetu watajifunza jinsi ya
kufanya upasuaji wa kuondoa vivimbe vya mishipa ya damu kwenye ubongo (Celebral
aneurysm) kwa mara ya kwanza hapa nchini ,kabla ya hapo wagonjwa walilazimika kwenda nje
ya nchi kwa gharama kubwa ” Alisema Dkt Boniface.
Dkt Boniface amesema gharama za upasuaji huu nje ya nchi ni zaidi ya Tsh milioni 60 na hapa
nchini haitazidi Tsh milioni 10 hivyo kuanza kwa huduma hii kutaokoa fedha nyingi za Serikali
na tayari Serikali imeshanunua darubini maalum ya kufanyia upasuaji huu mkubwa.
Mkurugenzi Mtendaji wa MOI Dkt Respicious Boniface akitoa neno la ukaribisho katika kongamano la kimataifa la madaktari bingwa wa upasuaji wa Ubongo, Mgongo na mishipa ya fahamu.
Aidha, Dkt. Roger Hartl Mkurugenzi wa Kitivo cha upasuaji wa Ubongo, Mgongo na Mishipa ya
fahamu kutoka chuo kikuu cha Weill Cornell amesema ni heshma kubwa kufika Tanzania kwa
mara nyingine, pia kupata fursa ya kubadilishana uzoefu na madaktari wa Tanzania na nchi
nyingine duniani.
“Pamoja na mafunzo ya nadharia tutafanya upasuaji kwa pamoja kwa njia za kisasa, hili ndilo
lengo letu hasa la kuja hapa, tunataka wenzetu wa MOI na madaktari walio mafunzoni waweze
kutoa huduma hizo kwa weledi mkubwa, tumekuwa tukifanya hivi kwa muda sasa na tunaona
wanakwenda vizuri hii inatia faraja sana” alisema Dkt Hartl.
Pia, Dkt. Hartl amesema mafunzo ya mwaka huu yanalenga kuwajengea uwezo washiriki ili
waweze kutumia teknoljia ya kisasa ya matibabu ya Ubongo na mgongo na kuwapa mbinu mpya
za upasuaji hususani kwa mgonjwa aliyeumia kwenye eneo la mfumo wa fahamu hususani
kwenye ubongo , uti wa Mgongo na mishipa ya fahamu iliyoharibika.
Taasisi ya MOI imeendelelea kufanya mageuzi makubwa katika huduma zake kwa lengo la
kuhakikisha huduma zote za kibingwa zinapatikana hapa nchini na kuendelea kuokoa maisha ya
watanzania na nchi nyingine za Afrika ambazo zinazoleta wagonjwa kutibibiwa MOI.
Kiongozi wa jopo la wakufunzi kutoka chuo kikuu cha Weill Cornel cha marekani
Prof Roger Hartl akiwasilisha mada katika kongamano la kimataifa la madaktari
bingwa wa upasuaji wa Ubongo ,Mgongo na Mishipa ya fahamu.
Mkurugenzi wa Ubora na Uhakiki kutoka Wizara ya Afya Dkt Mohamed Mohamed
wapili kutoka kushoto aikwa katika picha ya pamoja na washiriki wa kongamano
kutoka mataifa mbalimbali. Wakwanza kushoto ni Profesa Charles Mkonyi
mwenyekiti wa bodi ya wadhamini MOI, watatu kutoka kushoto ni Mkurugenzi
Mtendaji wa MOI Dkt Respicious Boniface na wakwanza kulia ni Kiongozi wa jopo
la wakufunzi kutoka marekani Profesa Roger Hartl.
No comments:
Post a Comment