HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, October 17, 2018

NAIBU WAZIRI NDITIYE ATEMBELEA MRADI WA DGMP BANDARINI


Na Leonard Magomba
Dar es Salaam: Oktoba 16, 2018. Mradi mkubwa wa kuboresha Bandari ya Dar es Salaam ‘Dar es Salaam Maritime Gateway Program’ (DGMP) umefikia asimilia 42 ya ujenzi wake hadi sasa.

Mradi huo unahusisha ujenzi wa gati maalum ya kushushia magari (RORO), gati Na. 1-7, kuongeza kina cha maji katika magati hayo pamoja na kutanua lango la kuingia meli bandarini.

Mradi huo ambao umelenga kuifanya Bandari ya Dar es Saalam kuwa ya kisasa zaidi na kuongeza uwezo wake wa kuhudumia meli kubwa kwa wakati mmoja unatarajia kukamilika mwezi Juni, 2020.

Hayo yamebainika leo wakati Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye alipotembelea mradi huo bandarini ili kukagua maendeleo ya ujenzi wake.

“Nimefurahishwa na maendeleo ya ujenzi wa mradi huu ambao hadi sasa umefikia asilimia 42 amesema Mh. Nditiye na kuongeza kwamba matarajio yetu mradi huu utaisha kwa wakati uliopangwa.”

Naye Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mhandisi Karim Mattaka amesema kwamba mradi huo bado upo ndani ya wakati pamoja na changamoto kadhaa zilizojitokeza wakati wa ujenzi wake.

Mhandisi Mattaka amesema kwamba kulikuwa na changamoto kadhaa wakati wa zoezi la kuhamisha mchanga (land reclamation) ambapo ilibainika kuna mchanga laini sana upo eneo litakalojengwa gati ya kushushia magari (RORO) hivyo kulazimika kuendelea na ujenzi wa gati namba 1 wakati zoezi la kutibu mchanga huo laini linaendelea.

“Ujenzi wa gati hili (namba 1) umefikia pazuri kwani unatarajiwa kukamilika mwishoni wa mwezi Disemba mwaka huu (2018) na hivyo kuanza kutumika rasmi kabla ya kuhamia gati namba 2,” amesema Mhandisi Mattaka.

Ujenzi wa gati ya RORO unatarajia kuanza mara baada ya zoezi la kutibu mchanga laini kukamilika. Mradi mzima wa maboresho hayo ya Bandari unatarajia kukamilika mnamo mwaka 2020.
 Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mhandisi Karim Mattaka akimkaribisha Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye mara baada ya kuwasili eneo la bandarini kukagua ujenzi wa mradi wa maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam.

Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mhandisi Karim Mattaka akitoa maelezo kwa Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye kuhusu ujenzi wa maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam alipofika eneo la kutengenezea zege linalotumika kwa ajili ya ujenzi huo.
 Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mhandisi Karim Mattaka akitoa maelezo kuhusu ujenzi wa gati namba moja (1) ya Bandari ya Dar es Salaam kwa Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye mara baada ya Waziri huyo kufanya ziara bandarini kukagua mradi huo.
 Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye akichanganya udongo katika maabara ya kuchanganyia udongo iliyopo bandarini kwa ajili ya zege la kujengea ujenzi unaoendelea kwa ajili ya mradi wa maboresho ya bandari ya Dar es Salaam. Anayeshuhudia kwa nyuma yake ni Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mhandisi Karim Mattaka.
Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mhandisi Karim Mattaka akitoa maelezo kuhusu ujenzi wa maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam kwa Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye mara baada ya kufika katika moja ya maabara zinazotumika kupima udongo kwa ajili ya ujenzi huo bandarini.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad