HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, September 1, 2018

TRENI YA KIFAHARI DUNIANI YALETA WATALII 64 DAR KUPITIA RELI YA TAZARA

 Fatma Salum- MAELEZO
TRENI ya kifahari inayojulikana kwa jina la ROVOS ambayo ni miongoni mwa treni tatu bora duniani imewasili jijini Dar es Salaam kwa kutumia reli ya Tazara ikiwa na watalii 64

Watalii hao wamekuja Tanzania kwa ajili ya kutembelea maeneo mbalimbali yenye vivutio vya utalii hapa nchini ikiwemo mbuga za wanyama na visiwa vya Zanzibar.

Akizungumza katika hafla fupi ya kuwapokea watalii hao iliyofanyika stesheni ya TAZARA Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa TAZARA Tanzania, Fuad Abdallah alieleza kuwa treni hiyo iliondoka mji wa Cape Town nchini Afrika ya Kusini Agosti 18, mwaka huu.

“Watalii mbalimbali huja nchini mara tano kwa mwaka kwa kutumia ROVOS kupitia reli ya TAZARA na nchi yetu hunufaika na ujio huu hasa faida za kiuchumi,” alisema Fuad.

Aidha alibainisha kuwa treni ya ROVOS ni miongoni mwa treni tatu bora duniani, hivyo ujio wa treni hiyo na watalii unatokana na vivutio bora vya utalii na miundombinu mizuri ya reli ya TAZARA.

“Treni hii inatumia reli ya TAZARA kuleta watalii kwa sababu nchi yetu imekidhi vigezo vya utalii na reli yetu imekidhi vigezo vya usalama na mawasiliano ya uhakika,” aliongeza Fuad. 

Alisema kuwa katika safari hiyo ya treni watalii hao pia walipata fursa ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Selous iliyopo kusini mwa Tanzania na kuona wanyama mbalimbali wanaopatikana kwenye hifadhi hiyo.

Wakizungumza kwa furaha ya kuwasili Tanzania, watalii hao wa kijerumani walisema kuwa wamefurahia sana safari hiyo na mapokezi mazuri ya watanzania na kuahidi kurudi kwa mara nyingine.

Kwa upande wake mfanyakazi wa treni ya ROVOS, Monica Rieder mwenye asili ya Ujerumani alisema kuwa amewahi kufika Tanzania mara 14 na anavutiwa na mabadiliko makubwa ya kimaendeleo yanayofanyika hapa nchini siku hadi siku.

TAZARA ni shirika la reli ya pamoja ya Tanzania na Zambia iliyoanza mwaka 1976 na inamilikiwa kwa asilimia 50 kila upande.


 Meneja Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania na Zambia (TAZARA) Fuad Abdallah (kulia), akizungumza na Waandishi wa Habari katika makao makuu ya shirika hilo Jijini Dar es Salaam kabla ya kuwasili kwa treni ya kitalii ya ROVOS kutoka Afrika ya Kusini.
 Baadhi ya watalii kutoka Ujerumani wakifurahia buradani ya bendi ya Polisi baada ya kushuka kutoka kwenye treni ya ROVOS moja kati ya treni ya kifahari duniani, watalii hao wamekuja nchini kutembelea vivutio mbalimbali.
Meneja Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania na Zambia (TAZARA) Fuad Abdallah (mwenye fulana nyekundu) akifuatilia mahojiano baina ya watalii na Afisa Habari wa Idara ya Habari-MAELEZO, Abraham Nyantori.
  Mtalii Diesknahn akizungumza na Afisa Habari wa Idara ya Habari Fatma Salum (kushoto) mara baada ya kuwasili nchini na treni ya ROVOS wakitokea Afika ya Kusini.
 Mama wa Kijerumani Linde Erdmann (katikati) akifurahia kuwasili Tanzania kwa mara ya kwanza akitokea Afrika ya Kusini kwa kutumia treni ya ROVOS kupitia reli ya TAZARA.
Moja ya mgahawa unaopatikana katika treni ya kifahari ya ROVOS iliyowasili leo hapa nchini ikitokea Afrika ya Kusini kupitia reli ya TAZARA.
Dereva wa treni ya ROVOS Abby (kulia) akizungumza na mmoja wa wafanyakazi wa treni hiyo mara baada ya kuwasili katika stesheni ya Dar es Salaam ikitokea Afrika  ya kusini kupitia reli ya TAZARA.
 Moja ya chumba cha kupumzika abiria katika treni ya kifahari ya ROVOS, treni hiyo ni miongoni mwa treni tatu za kifahari duniani.
  Treni ya ROVOS iliyobeba watalii 64 wa Kijerumani kutoka Afrika ya Kusini, ikiwasili leo stesheni ya TAZARA Jijini Dar es Salaam.
(Picha na Paschal Dotto- MAELEZO).

1 comment:

  1. its ny first time to hear this i thought it is a jock Nice to hear that

    ReplyDelete

Post Bottom Ad