HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 20, 2018

POLISI ARUSHA WAFANIKIWA KUPATA GARI AINA YA TOYOTA SURF ILIYOIBIWA SEPTEMBA 17

Na Seif Mangwangi, Arusha
JESHI la Polisi Mkoa wa Arusha limefanikiwa kupata gari aina ya Toyota surf namba T996AGK, lililokuwa limeibiwa  Septemba 17, mwaka huu katika eneo la stand ndogo lilipokuwa limepakiwa.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Ramadhan Ng'azi alisema dereva wa gari hilo Susan Cornel mwalimu wa shule ya msingi Maviluni Akeri alikuwa amepaki gari hilo na kuingia stand kwa ajili ya kufanya manunuzi.

Anasema aliporejea alikuta gari lake halipo ndipo akatoa taarifa polisi na wao kuanza harakati za kulisaka gari hilo kwa kuweka vizuizi maeneo mbalimbali na baadae kupata taarifa kuwa gari hilo limetelekezwa eneo la kituo cha afya Kaloleni.

Kamanda Ng'azi amesema jeshi hilo linaendelea kuchukua alama mbalimbali ili kuweza kubaini wezi walioliiba na kulitelekeza.

Katika taarifa yake ya pili Kamanda N'gazi alisema jeshi hilo limefanikiwa kukamata bastola moja aina ya browning  na risasi nane ikiwa imehifadhiwa katika chumba cha mkazi mmoja katika eneo la Kimnyak ambapo mtuhumiwa huyo ambae jina lake halijaweza kupatikana  alitoroka baada ya kupata taarifa anatafutwa.

Wakati huo huo Kamanda wa Jeshi la uhamiaji Mkoa wa Arusha  Samweli Maharane amesema kwa kushirikiana na jeshi la polisi Septemba 12, mwaka huu walimkamata raia mmoja wa ubelgiji Catherine Degrave mwenye passport namba EN298121 akifananishwa na mtuhumiwa mmoja raia wa sweden Susan Nordun  aliyewahi kufukuzwa nchini.

Amesema raia wema walitoa taarifa za kuwepo kwa mwanamke huyo ambaye hata hivyo baada ya kumfanyia uchunguzi waligundua sio Susan aliyedhaniwa licha ya kufanana sana na mtuhumiwa huyo na hivyo kumruhusu kuendelea na shughuli zake.
  Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Ramadhani Ng'azi akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mali mbalimbali zilizokamatwa na kuwataka wakazi wa Arusha kufika ofisini kwake kwa ajili ya kutambua mali walizoibiwa.
 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Ramadhani Ng'azi akionyesha mali mbalimbali zilizokamatwa na kuwataka wakazi wa Arusha kufika ofisini kwake kwaajili ya kutambua mali walizoibiwa.
Mwalimu Susan Cornel mkazi wa Olasiti Arusha akizungumza na waandishi wa habari nje ya Makao makuu ya Polisi Arusha akieleza namna gari lake liliibiwa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad