HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, September 18, 2018

LUKUVI ALILIWA ZUMBA /SOGA KUTATUA MGOGORO WA ARDHI BAINA YA WANANCHI NA MWEKEZAJI

NA MWAMVUA MWINYI,KIBAHA VIJIJINI

MBUNGE wa jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa, ameingilia kati mgogoro wa ardhi kati ya kampuni ya Mohammed Enterprises na kijiji cha Zumba ,Mpiji Stesheni ,Soga na Kipangege huku akimuomba Waziri mwenye dhamana kutatua mgogoro huo.

Aidha ,amelazimika kuunda kamati ndogo ya watu 12 ,itakayofuatilia jambo hilo ili haki itendeke .

Akizungumza na wananchi hao ,Jumaa alisema, ifikie hatua ya wataalamu na viongozi wenye dhamana kukutana na wananchi ,kuwaeleza jitihada zinazochukuliwa na serikali kutatua malalamiko yao bila kukaa kimya .

"Tatizo hili nimelikuta ,katika kipindi changu ni miaka saba sasa ,2015 niliongea na waziri na kuja na kamati ya ardhi ,na kutolewa maelekezo mbalimbali lakini bahati mbaya ,wakati wa uchaguzi ule waziri husika hakuweza kufika "

"Mkuu wa wilaya ya Kibaha aliwahi kufika kuongea na wananchi ,na mkoa wa Pwani ulifikishiwa hatua zinazochukuliwa walitumwa wataalamu kufanya tathmini na kujua mapungufu ya ardhi ya wananchi wanayohitaji ." alisema Jumaa.

Jumaa alieleza ,tangu hapo hakuna taarifa ya hatua hizo zilipofikia lakini amejipanga kufuatilia suala hilo kwa kushirikiana na kamati iliyoundwa .

"Mh Lukuvi ni mwelewa na ana hekima , naamini atalitatua tatizo hili bila kuangalia upande wowote ,ili kuondoa dhana ya wananchi kuwa mwekezaji kaiweka serikali mfukoni " alifafanua Jumaa.


Hata hivyo ,Jumaa alikemea tabia inayofanywa na meneja wa mwekezaji huyo aitwae Mndeme kunyanyasa baadhi ya wananchi na wengine kupigwa na kupelekwa polisi bila hatia .

Alimuasa kuacha kuchukua sheria mkononi ,kwani alishawahi kupigwa mtu hadi kufa katika shamba hilo.

Awali mkazi wa kijiji cha Zumba ,Joseph Massana alisema inatia shaka kwa viongozi kupata kigugumizi, kushindwa kutatua tatizo hilo .

"Mwekezaji ana jumla ya hekari 25,000 ambazo aliuziwa wakati wa ubinafsishaji ambao umefuta haki zote za wananchi aliowakuta " alifafanua Massana.

Nae mwenyekiti wa kijiji cha Mpiji Stesheni ,Saidi Abdallah alisema wananchi wawe na imani na subira kusubiria hatua zinazochukuliwa na mbunge.

Alielezea kwamba ,tangu azaliwe ni miaka 40 huku maeneo hayo yakiwepo na mwekezaji haendelezi lolote .

Abdallah aliomba ,serikali iingilie kati kumaliza tatizo hili ,kwakuwa hakuna maendeleo ya kijamii yanayofanyika hadi hapo suluhu itakapopatikana.
 Mbunge wa jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa ,akizungumza na wananchi kijiji cha Zumba kuhusiana na mgogoro wa ardhi kati ya wananchi na kampuni ya Mohammed Enterprises.
Mwenyekiti wa kijiji cha Mpiji Stesheni ,Saidi Abdallah akizungumza katika mkutano na wananchi kuelezea mgogoro wa ardhi.
 (Picha na Mwamvua Mwinyi)

2 comments:

  1. Jamani toka enzi hizo bado mgogoro huo haujapatiwa uvumbuzi, hivi kuna nini? Ama ndo mwekezaji kaweka serikali mufukoni? Wanyonge tunateseka...

    ReplyDelete

Post Bottom Ad