Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imeombwa kuwafikia
wananchi wengi zaidi wakiwemo wafanyakazi ili waweze kufanyiwa vipimo vya
moyo pamoja na kupata elimu ya jinsi ya kuepukana na ugonjwa huo.
Ombi hilo limetolewa leo na washiriki wa mkutano wa mwaka wa wahandisi
uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Diamond Jubilee uliopo jijini Dar es
Salaam.
Wahandishi hao pia wamewashauri wafanyakazi kutenga muda wa kupima afya
zao na kufanya mazoezi ambayo yatawasaidia kiafya.
Mhandisi Alex Kalanje alisema kama Taasisi hiyo itawafikia watu wengi zaidi kwa
kwenda katika mikusanyiko mbalimbali kutawasaidia watanzania wakiwemo
wafanyakazi ambao kutokana na majukumu yao ya kazi wanakosa muda wa
kwenda kupima afya zao kupata huduma ya uchunguzi wa magonjwa ya moyo.
“Wafanyakazi wengi wanakosa muda wa kwenda Hospitali kupima afya zao, lakini
kama kutakuwa na utaratibu wa kuwepo kwa wataalam wa afya katika mikutano
mbalimbali kutawasaidia kupata muda wa kupima kirahisi zaidi kuliko
wanapokuwa katika maeneo yao ya kazi”, alisema Mhandisi Kalanje..
Kwa upande wake Mhandisi Dkt. Gemma Modu aliwashauri watanzania kutenga
muda wa kupima afya zao kwa kufanya hivyo kutawasaidia kujuwa kama
wanamatatizo au la na kama wanayo wataweza kupata matibabu mapema.
Aidha Dkt. Gema pia aliwasihi kinamama kubadilika na kuhamasisha familia zao
kwenda kupima na ikifika muda wa kupima waende wao na waume zao pamoja
na watoto.
Akizungumza wakati wa kufungwa kwa mkutano huo Naibu Katibu Mkuu wa
Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Dkt. Jim James Yonazi aliipongeza
Taasisi ya Moyo kwa huduma ya kijamii iliyoitoa ya upimaji na kutoa elimu ya
lishe pamoja na mazoezi na kusema kuwa kazi waliyoifanya ni kubwa.
Taasisi hiyo ilishika nafasi ya kwanza ya mtoa huduma za kitaalam kwa kutoa
huduma za upimaji wa vihatarishi vya magonjwa ya Moyo, ushauri wa kiafya
kuhusiana na Magonjwa ya Moyo, elimu ya lishe bora na mazoezi, kueleza kwa
kina huduma zinazotolewa na Taasisi, kutoa dawa bure kwa watu waliokutwa na
matatizo ya moyo na kutoa rufaa ya moja kwa moja kwa wagonjwa waliokutwa na
matatizo ya moyo yaliyohitajika kupewa rufaa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof.
Mohamed Janabi akipokea cheti cha nafasi ya kwanza ya mtoa huduma za kitaalam kutoka
kwa Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe. Elias Kwandikwa
kutokana na Taasisi hiyo kushiriki katika kutoa huduma ya upimaji wa magonjwa ya moyo
kwenye mkutano wa wahandisi uliofanyika katika ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es
Salaam.
Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dorica Burengelo
akimpima ugonjwa wa kisukari mhandisi aliyetembelea banda la hiyo kwa ajili ya kupima
afya na kupata elimu ya lishe na mazoezi wakati wa mkutano wa 16 wa wahandisi uliofanyika
katika ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es Salaam.
Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Theophylly Mushi
akimpima msukumo wa damu (PB) mhandisi aliyetembelea banda la Taasisi hiyo kwa ajili ya
kupima afya na kupata elimu ya lishe na mazoezi wakati wa mkutano wa 16 wa wahandisi
uliofanyika katika ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es Salaam.
Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hussein Mube akimpa
ushauri wa kiafya mhandisi aliyetembelea banda la Taasisi hiyo kwa ajili ya kupima afya na
kupata elimu ya lishe bora na mazoezi wakati wa mkutano wa 16 wa wahandisi uliofanyika
katika ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es Salaam.
Washiriki wa upimaji afya, utoaji wa elimu ya lishe bora na mazoezi wakiwa
katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Prof. Mohamed Janabi mara baada ya kupokea cheti cha kushika nafasi ya kwanza ya mtoa
huduma za kitaalam kwenye mkutano wa wahandisi uliofanyika katika ukumbi wa Diamond
Jubilee Jijini Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment