HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 6, 2018

DC SOPHIA MFAUME AHIMIZA WADAU WA MAENDELEO KUWEKEZA WILAYANI NAMTUMBO

Na Ripota Wetu, Globu ya jamii
MKUU wa Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma Sofia Mfaume amesema kuna kila sababu ya sekta binafsi na sekta za umma kushirikiana kuhakikisha Wilaya hiyo na Taifa kwa ujumla inapiga hatua kimaendeleo.

Amesema sekta hizo zikishirikiana katika kutatua changamoto zilizopo katika baadhi ya maeneo ya Wilaya ya Namtumbo wananchi watapiga hatua kubwa kimaendeleo huku akiomba sekta binafsi kuwekeza ndani ya wilaya hiyo.

Mfaume amesema hayo leo wakati wa mkutano kati ya sekta binafsi na sekta za umma wilayani Namtumbo.

Amesema lengo la mkutano huo ni wadau wa maendeleo kupitia sekta hizo kujadili na kuweka mikakati ya kutatua changamoto na kisha kufanya maendeleo.

Amewaambia wadau wa maendeleo ni vema wakatambua Wilaya ya Namtumbo kuna fursa nyingi ambazo zikitumika vizuri kutakuwa na maendeleo.

“Wilaya yetu ya Namtumbo tunayo ardhi ya kutosha na yenye rutuba inayokubali mazao ya kila aina.Wananchi wanaitumia vema ardhi iliyopo katika kujiletea maendeleo.

“Ombi langu kwa wadau wa sekta zote hizi tushirikiane katika kuleta maendeleo na kwetu tutafurahi tukiona viwanda vinajengwa zaidi na hasa vya kuongeza thamani ya mazao ya wakulima,”amesema Mfaume.

Baadhi ya wananchi wa Wilaya ya Namtumbo ambao wamepata nafasi ya kuuzungumzia mkutano huo wamesema unaonesha matumaini makubwa ya kupatikana kwa maendeleo ndani ya wilaya yao na zaidi wanampongeza Mkuu wao wa Wilaya kwani amekuwa chachu ya maendeleo ya wananchi.
Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo Sophia Mfaume akizungumza wakati wa mkutano kati ya sekta binafsi na sekta za umma uliofanyika wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma leo

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad