HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, September 2, 2018

BARABARA YA MASWA-BARIADI KUONGEZA UKUAJI WA UCHUMI KANDA YA ZIWA

Ujenzi unaondelea wa barabara ya Maswa-Bariadi yenye urefu wa Km 49.7 kwa kiwango cha lami unatarajiwa kufungua mkoa wa Simiyu na mikoa jirani ya Mara, Mwanza na Shinyanga hivyo kutarahisisha usafirishaji wa abiria na mizigo. Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe mkoani Simiyu wakati akikagua barabara hiyo inayojengwa na mkandarasi wa kampuni ya CHICO na kuridhishwa na hatua zilizofikiwa katika ujenzi huo toka ulipoanza mwezi Oktoba mwaka 2017.

"Nimeridhishwa na hatua zilizofikiwa na nina imani mkandarasi atamaliza mapema mradi huu",amesisitiza Waziri Kamwelwe. Aidha, ameupongeza uongozi wa mkoa huo na Wakala wa Barabara (TANROADS), kwa kusimamia mradi huo usiku na mchana na kuwataka kutoa taarifa muda wowote endapo kutakuwa na changamoto zinazoweza kukwamisha mradi huo.
Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Simiyu Mhandisi Albert Kent, akimuoesha Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe, nyumba za Mhandisi Mshauri zilizojengwa na mkandarasi wa Kampuni ya CHICO katika mradi wa ujenzi wa barabara ya Maswa-Bariadi yenye urefu wa KM 49.7 kwa kiwango cha lami, mkoani humo.

Akizungumzia kuhusu Kiwanja cha Ndege cha Simiyu, Mhandisi Kamwelwe amemueleza Mkuu wa Mkoa kuwa hatua za awali zinaendelea katika kuhakikisha kiwanja hicho kinajengwa ili kufungua mkoa huo katika sekta za usafirishaji na uwekezaji.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka, ameishukuru Serikali kwa kujenga kipande cha barabara hiyo baada ya ile ya Mwigumbi-Maswa kukamilika kwa kiwango cha lami kwa kuwa imekua ni kichocheo cha kuunganisha nchi yetu na nchi za maziwa makuu ambazo ni Uganda, Burundi, Rwanda, Kenya na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo(DRC).
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe, na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka wakikagua kokoto zitakazotumika katika ujenzi wa barabara ya Maswa-Bariadi yenye urefu wa KM 49.7 kwa kiwango cha lami, Mkoani humo.

Naye, Meneja wa TANROADS Mkoa wa Simiyu Mhandisi Albert Kent amemueleza Waziri huyo kuwa mradi huo mpaka sasa umefikia asilimia 20 na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Oktoba mwaka 2019.

Mhandisi Kent ameongeza kuwa kazi zilizofanyika mpaka sasa ni mkandarasi kuanza ujenzi wa madaraja makubwa mawili ya Banhaya na Simiyu na ameshamaliza kujenga madaraja madogo 9 kati ya 12 na makalvati 36 kati ya 58.

Mradi wa Maswa-Bariadi unagharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa asilimia 100 na unatarajiwa kugharimu zaidi ya shilingi Bilioni 86. Kukamilika kwa mradi huo kutakamilisha ujenzi wa barabara ya Mwigumbi-Maswa- Bariadi-Lamadi yanye jumla ya urefu wa KM 171.8.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe, akioneshwa na Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Simiyu Mhandisi Albert Kent, kazi zinazoendelea katika ujenzi wa daraja la mto Simyu, wakati alipofanya ziara ya ukaguzi wa ujenzi wa barabara ya Maswa-Bariadi yenye urefu wa KM 49.7 kwa kiwango cha lami, Mkoani humo. 
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe, akifafanua jambo kwa Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka wakati alipofanya ziara ya ukaguzi wa ujenzi wa barabara ya Maswa-Bariadi yenye urefu wa KM 49.7 kwa kiwango cha lami, Mkoani humo.
Muonekano wa kazi za ujenzi zikiendelea kwenye daraja la mto Simiyu katika barabara ya Maswa-Bariadi yenye urefu wa KM 49.7, Mkoani Simiyu.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad