HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 10, 2018

MIKOA YA GEITA, NJOMBE, RUKWA NA SIMIYU KUPATA VYUO VYA VETA


Uongozi wa Wilaya na Halmashauri ya Chato, Uongozi wa VETA,Wakandarasi na baadhi ya wananchi wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa makabidhiano ya eneo la ujenzi wa chuo cha Wilaya hiyo kwa Mkandarasi.
Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel (Kushoto)alitazama mwonekano katika picha wa Chuo cha Mkoa huo pindi kitakapomaliza.
Mwenyekiti wa Bodi wa Bodi ya VETA Ndg. Peter Maduki akikabidhi mchoro wa chuo cha VETA Geita kwa mkandarasi wa kampuni ya Skywards Construction aliyepewa kazi ya ujenzi wa chuo hicho
Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel (kushoto) akizungumza na Mwenyekiti wa Bodi ya VETA Ndg.Peter Maduki wakati wa makabidhiano ya eneo la ujenzi wa Chuo cha VETA cha Mkoa wa Geita.Wengine ni Wakurugenzi wa VETA na wakandarasi wa mradi huo.

SERIKALI kupitia Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imeanza utekelezaji wa  ujenzi wa Vyuo vya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi kwa Mikoa ya Geita, Njombe, Rukwa na Simiyu ikiwa ni sehemu ya kutoa huduma ya ufundi na ujuzi ili kukidhi mahitaji ya mikoa hiyo.

Akizungumza wakati wa hafla fupi ya kukabidhi maeneo ya ujenzi wa vyuo vya mkoa wa Geita na Wilaya ya Chato, Mwenyekiti wa Bodi ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi Peter Maduki  alisema  ujenzi wa vyuo hivyo kwa mikoa hiyo una lengo la kutekeleza mkakati wa Mamlaka wa  kuongeza udahili hadi kufikia idadi ya wanafunzi 700,000 ifikapo mwaka 2020.

Alisema kuwa jitihada hizo zinaenda sanjari na utekelezaji wa nia njema ya Serikali ya awamu ya tano ya kuhakikisha kuwa vijana wanapata ujuzi stahiki utakaowawezesha kuajiriwa au kujiajiri ili kushiriki kikamilifu katika kukuza uchumi na kuhakikisha nchi inafikia uchumi wa kati ifikapo 2025.

Akikabidhi rasmi nyaraka za ujenzi wa Chuo cha Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) cha Mkoa wa Geita chenye ukubwa wa hekta 27 kwa Mkandarasi anayejenga chuo hicho Kampuni ya Kitanzania Skywards Construction
 mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel, Maduki alisema kuwa gharama ya ujenzi wa chuo hicho ni kiasi cha Sh bilioni 9.9 fedha za mkopo kutoka benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).

Kwa upande wa chuo cha Wilaya ya Chato, alisema ujenzi wake utagharimu kiasi cha  Sh bilioni 10.7 ambazo ni fedha za ndani na ujenzi utafanywa na kampuni ya Kitanzania ya  C.F Builders yenye makao yake jijini Mwanza.

Alisema vyuo hivyo vitakapokamilika vitakuwa na uwezo wa kudahili jumla ya wanafunzi 2940, ambapo kwa chuo cha mkoa wa Geita pekee  kitakuwa na uwezo wa kudahili wanafunzi 660 kwa ngazi tatu kwa mafunzo ya muda mrefu kwa mwaka na wanafunzi wasiopungua 1000 kwa mafunzo ya muda mfupi huku Chuo cha VETA Chato chenye ukubwa wa ekari 70  kitakuwa na uwezo wa kudahili wanafunzi 480 kwa ngazi hizo tatu za mafunzo ya muda mrefu na wanafunzi wasiopungua 800 kwa mafunzo ya muda mfupi.

Alizitaja baadhi ya fani zitakazotolewa katika vyuo hivyo kuwa ni pamoja na Ufundi wa Mitambo Mizito, Ufundi Elektroniki, Mechatronic,Ufundi Umeme wa Magari,Ufundi Uashi,Ufundi Umeme, Ufundi bomba, Ukarimu na Usindikaji wa Samaki,Useremala, Mafunzo ya Uhazili na Compyuta na Ufundi wa vifaa tiba.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel alimshukuru Rais John Magufuli kwa kazi kubwa anayofanya ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali nchini sambamba na ujenzi wa vyuo hivyo vya kisasa ambavyo vitawawezesha wananchi hasa vijana kupata ujuzi ili waweze kujiajiri sanjari na kuwavutia wawekezaji kwenda kuwekeza mkoani kwake.

Aliushauri uongozi wa VETA kutoa kipaumbele kwa fani zinazohusiana na teknolojia ya uchimbaji ili kuwawezesha wachimbaji wadogo kuchimba madini kitaalam na kuongeza tija katika shughuli hiyo inayofanywa na vijana wengi mkoani Geita.

Aliwataka wakandarasi wa miradi hiyo kuhakikisha kuwa wanakamilisha kazi ya ujenzi kwa muda uliopangwa kwa kuwa wananchi wa mkoa wa Geita wana matarajio makubwa ya kuona miradi hiyo inakamilika kwa wakati mwafaka na kwa ubora unaotarajiwa.   

“Nitakuwa nakagua ujenzi wa miradi hii mara kwa mara ili kuona utekelezaji wake”, alisema.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Chato Elias Makori aliishukuru serikali kwa kuamua kujenga chuo hicho wilayani Chato ambacho alisema kitaongeza ajira, ujuzi kwa vijana sanjari na kupunguza umaskini

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato Batholomeo Manunga alisema ujio wa mradi wa ujenzi wa chuo hicho utatatua changamoto ya ajira kwa vijana ambao watapata ujuzi utakaowawezesha kuajiriwa na kujiajiri na kukuza vipato vyao.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad