HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, August 18, 2018

JKCI kwa kushirikiana na Kampuni ya Merck waandaa mkutano wa kwanza wa kutathimini magonjwa ya moyo nchini

Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Delila Kimambo akielezea jinsi mashine ya kupima moyo (Echocardiogram) inavyofanya kazi ya kutambua matatizo yaliyopo katika moyo wakati wa mkutano wa kwanza wa kitaifa wa kutathmini magonjwa ya moyo nchini uliofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa JKCI uliopo Jijini Dar es Salaam.

Na Salome Majaliwa - JKCI

Madaktari wa Hospitali za Rufaa nchini wameshauriwa kuwatuma mapema wagonjwa wa moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) pindi wanapowapima na kugundulika kuwa na ugonjwa huo ili waweze kupatiwa matibabu mapema.

Rai hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi ambaye pia ni Daktari bingwa wa magonjwa ya Moyo kutoka JKCI Delila Kimambo wakati wa mkutano wa kwanza wa kitaifa wa kutathmini magonjwa ya moyo nchini uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo.

Dkt. Delila alisema wagonjwa wa moyo wanaotibiwa katika Hospitali mbalimbali hapa nchini rufaa yao huwa ni Taasisi ya Moyo hivyo basi ni muhimu wagonjwa hao wakafika katika Hospitali hiyo kwa wakati.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Shirika la Madaktari Afrika la nchini Marekani Prof.Matthew Sackett akielezea jinsi mtambo wa Cathlab unavyotumika kutibu na kupima magonjwa ya moyo wakati wa mkutano wa kwanza wa kitaifa wa kutathmini magonjwa ya moyo uliofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) uliopo jijini Dar es Salaam.

“Wagonjwa wengi tunaowapokea mioyo yao huwa imechoka, kama wagonjwa hawa wangefika mapema kwetu wangepata matibabu madogo kuliko kupatiwa matibabu makubwa ya upasuaji wa kifua au bila kufungua kifua kwa kutumia tundu dogo”.

“Kutokana na wagonjwa wengi kuchelewa kufika hospitalini ama kutokupata matibabu ya moyo kwa wakati, tumeona tuwe na mafunzo haya hii itawasaidia madaktari wengi kupata ujuzi zaidi na kuweza kutambua wagonjwa kwa wakati”, alisema Dkt. Delila.

Akizungumzia kuhusu mkutano huo Dkt. Delila alisema lengo ni kuwapatia madaktari ujuzi hususani wa namna ya kupima moyo kwa kutumia mashine za ECHO na umeme wa moyo (Electrocardiography – ECG).

Kwa upande wake Daktari kutoka hospitali ya Amana Natalius Kapilima alisema mafunzo hayo yamewasaidia kupata ujuzi utakaowawezesha kuwatambua wagonjwa wa moyo kupitia vipimo vya ECHO na ECG.

Naye Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka hospitali ya Aga Khan Prof. Mustafa Bapuma aliishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa kuona mbali na kuwezesha kufanyika kwa mafunzo hayo kwa madaktari. Kupitia mafunzo hayo wataweza kutibu wagonjwa wa moyo kwa ustadi na ufanisi zaidi kuliko hapo awali.

Mkutano huo wa siku moja umeandaliwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa kushirikiana na Kampuni ya Merck ambapo jumla ya washiriki 80 kutoka Hospitali mbalimbali za mkoa wa Dar es Salaam walishiriki.
Baadhi ya Madaktari wa Magonjwa ya Moyo kutoka Hospitali mbalimbali za mkoa wa Dar es Salaam wakifuatilia mada ya jinsi ya kumtambua mgonjwa mwenye matatizo ya moyo kwa kupitia kipimo cha ECHO wakati wa Mkutano wa kwanza wa kitaifa wa kutathmini magonjwa ya moyo nchini uliofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) uliopo jijini Dar es Salaam. Picha na Genofeva Matemu - JKCI

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad