HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, July 24, 2018

Serikali kuimarisha soko la chumvi la ndani kwa kuzuia chumvi kutoka nje

Na Zuena Msuya, Pwani,
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo amesema Serikali kupitia Wizara ya Madini inaangalia namna bora ya kuimarisha soko la chumvi inayozalishwa nchini yenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya ndani na ziada, kwa kuzuia ile inayoingizwa kutoka nchi za nje.
Nyongo alisema hayo, wilayani Bagamoyo mkoani Pwani, Julai 23, 2018, baada ya kutembelea Mgodi wa kuzalisha chumvi wa kampuni ya Stanley and Sons ulioanzishwa mwaka 1948/49 uliopo katika Kijiji cha Kitame wilayani humo.
Akizungumzia uzalishaji chumvi, Nyongo alitolea mfano mgodi pekee wa Stanley kuwa, huzalisha chumvi kati ya tani 4000 hadi 6000 kwa mwaka kulingana na hali ya hewa, licha ya kuwepo migodi mingi ya uzalishaji chumvi katika baadhi ya Mikoa nchini ambapo mara nyingi wazalishaji wamekuwa wakilalamikia ukosefu wa soko la chumvi wanayozalisha.
Alitaja baadhi ya Mikoa iliyokuwa na migodi ya kuchimba na kuzalisha chumvi kuwa ni pamoja Pwani yenye zaidi ya mgozi mmoja, Kigoma katika eneo la Uvinza, Lindi pamoja na Mtwara.
" Tanzania ina migodi mingi ya kuchimba na kuzalisha chumvi bora, ya kutosha na yenye kukidhi mahitaji ya ndani na kuuza nje, hivyo ni wakati sasa, serikali kuangalia namna bora ya kulinda soko la ndani la chumvi kwa kuzuia ile inayoingizwa kutoka nje, ili wazalishaji waweze kupata soko la uhakika", alisisitiza Nyongo.
Aidha aliwaagiza wachimbaji na wazalishaji wa chumvi nchi, kusindika chumvi hiyo katika ubora unaotakiwa na kukidhi viwango vya soko la Kimataifa kwa kuzingatia kuwa, Tanzania inazalisha chumvi iliyobora.
Sambamba na hilo, alieleza kuwa kwakuwa chumvi ni bidhaa mtambuka inayotumika kama chakula, dawa, pamoja na kuwa ni madini hivyo, aliwataka wachimbaji na wazalishaji wa chumvi, kusindika chumvi hiyo katika ujazo tofauti na kwa bei nafuu ili kila mmoja aweze kumudu gharama za kununua chumvi hiyo kwa matumizi husika ikiwemo majumbani, viwandani na hata katika mifugo.
Pia, alisema wazalishaji wakubwa wawasaidie na kuwawezesha wafanyabiashara wadogo wa chumvi ili na wao waweze kuuza na kusambaza chumvi hiyo ili iwafikie watumiaji wa aina mbalimbali kwa urahisi zaidi na kukidhi mahitaji ya walaji kwa wakati.
" Watumiaji wengi wa chumvi majumbani wananunua na kutumia iliyosindikwa katika ile mifuko midogo ya robo au nusu kilo, sasa ninyi wachimbaji na wazalishaji wa chumvi muangalie namna ya kuwafikia watumiaji wote wa chumvi hapa nchini, hii italeta tija kwa watanzania kutangaza na kutumia bidhaa zinazozalishwa nchini", alisema Nyongo. 
Nyongo aliendelea kusisitiza kuwa, Serikali inaendelea kuunga mkono juhudi za wachimbaji na wazalishaji wa chumvi nchini kwa kuweka mazingira rafiki yanayowawezesha kufanya kazi hiyo katika kiwango kikubwa na ubora unaotakiwa.
Pamoja na mambo mengine, alisema kuwa, tayari serikali imewafutia wachimbaji na wazalishaji chumvi, kodi kumi na moja ambazo zilikuwa kero kubwa kwao, na kwamba serikali inaendelea kushughulikia vikwazo vingine vinavyokwamisha shughuli zao.
Aidha alitaja baadhi ya nchi zinazonunua chumvi ya Tanzania kuwa ni pamoja na Jamuhuri ya Watu Congo, Malawi, Msumbiji,pamoja na Uganda na kusema kuwa lengo ni kufikia nchi nyingi zaidi duniani. 
Aliwaagiza wachimbaji na wazalishaji wote wa chumvi nchini kulipa mirabaha na tozo mbalimbali na kushiki katika shughuli za kijamii zilizowekwa kwa mujibu wa sheria ya madini, kwa lengo la kuongeza pato la taifa kwa manufaa ya watanzania.
Mmoja wa Wakurugenzi katika Mgodi wa Chumvi wa Kampuni ya Stanley and Sons, Richard Stanley aliiomba serikali kuboresha miundombinu ya barabara itakayorahisisha usafirishaji ya chumvi hiyo, kwa kuwa katika kipindi cha wa mvua hakuna vyombo vya usafiri vinavyoweza kufika katika eneo hilo.
Vilevile, Richard aliiomba serikali kuwapelekea huduma ya umeme katika kijiji hicho ili kupunguza gharama za uzalishaji ambapo kwa sasa hutumia mafuta mazito kuendeshea mashine za uzalishaji.
Hata hivyo, Naibu Waziri Nyongo aliwahakikisha wawekezaji hao kuwa changamoto zote zitashughulikiwa katika kipindi kifupi kijacho kwa kuwa nia ya serikali ni kuwawezesha wawekezaji wa ndani na nje waweze kufanya shughuli zao katika mazingira mazuri na rafiki ili kuunga mkono azma ya serikali ya kuwa tanzania ya viwanda kutokana na rasilimali zilizopo nchini.
Naibu Waziri  Stanslaus Nyongo( aliyeinama) akigusa chumvi iliyorundikwa tayari kwa kufungashwa katika mifuko kwa ajili ya kuuzwa kwa watumiaji.
 Baadhi ya vitalu vya kuzalisha chumvi katika mgodi wa kampuni ya Stanley and Son, uliopo katika Kijiji cha Kitame wilayani Bagamoyo mkoani Pwani. 
Naibu Waziri,  Stanslaus Nyongo,(kulia) akiingia katika moja ya vitalu vya mgodi wa chumvi wa kampuni ya Stanley and Sons.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad