*Ataka apewe majina ya watakaokiuka agizo hilo
*Akataza magari ya Serikali kulala nyumbani kwa mtu
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewaagiza watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Bahi mkoani Dodoma wanaoishi nje ya eneo lao la kazi wawe wamehamia ifikapo Julai 30, mwaka huu.
“Tunataka watumishi wa umma wawajibike na waishi katika vituo vyao vya kazi. Nawataka watumishi wote wa wilaya hii wanaoishi Dodoma wawe wamehamia hapa ifikapo Julai 30 mwaka huu na wasiohamia nipewe majina yao,” amesisitiza.
Pia ameagiza magari yote ya Serikali baada ya kuisha muda ya kazi yawe yameegeshwa kwenye ofisi za halmashauri na ni marufuku kwa magari hayo kulala nyumbani kwa mtu.
Ametoa maagizo hayo leo (Jumatano, Juni 27, 2018) wakati akizinduavituo 51 vya kufuatilia taarifa za hali ya hewa, vituo 15 vya haidrolojia, kanzidata ya taarifa za hali ya hewa na kituo cha operesheni na mawasiliano ya dharura wilayani Bahi, Dodoma.
Waziri Mkuu amesema Serikali inataka watumishi wote wa umma nchini waishi kwenye vituo vyao vya kazi ili waweze kuwahudumia wananchi kwa ukaribu katika maeneo husika.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amemuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Bahi, Bibi. Rachel Chuwa aanzishe mradi wa upimaji wa viwanja na viuzwe kwa watumishi na wananchi kwa gharama nafuu.
Waziri Mkuu amesema ni vema wilaya hiyo ikachangamkia fursa ya Serikali kuhamia Dodoma kwa kuboresha miundombinu mbalimbali ikiwemo nyumba za kuishi, hoteli na sehemu za burudani ili watumishi waliohamia Dodoma wapate sehemu za kujipumzisha pindi wamalizapo majukumu yao.
Waziri
Mkuu Kassim Majaliwa akizindua vituo 51 vya kufuatilia taarifa za hali
ya hewa katika viwanja vya Ofisi ya Halmashauri ya wilaya ya Bahi
mkoani Dodoma Juni 27, 2018. Kulia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri
Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenista
Mhagama. Wanne kushoto ni Mwakilishi Mkaazi wa Mpango wa Maendeleo wa
Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bibi Natalie Boucly.
Waziri
Mkuu, Kassim Majaliwa akitazama chombo cha kupima wingi wa mvua baada
ya kuzindua vituo 51 vya kufuatilia taarifa za hali ya hewa katika
viwanja vya Ofisi ya Halmashauri ya wilaya ya Bahi mkoani Dodoma Juni
27, 2018. Wengine pichani kutoka kushoto ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya
Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu,Jenista
Mhagama,Waziri wa Maji, Mhandisi Isaack Kamwele, Mwakilishi Mkaazi wa
Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bibi Natalie
Boucly na kulia ni Mbunge wa Viti Maalum kutoka mkoa wa Dodoma, Felista
Bura. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Baadhi
ya wananchi walioshiriki katika uzinduzi wa vituo 51 vya kufuatilia
taarifa za hali ya hewa uliofanywa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa
katika viwanja vya Ofisi ya Halmashauri ya wilaya ya Bahi mkoani Dodoma
Juni 27, 2018.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akibonyeza kitufe wakati alipozindua vituo
51 vya kufuatilia taarifa za hali ya hewa katika viwanja vya Ofisi ya
Halmashauri ya wilaya ya Bahi mkoani Dodoma Juni 27, 2018. Kulia ni
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge,Kazi, Vijana, Ajira na
Wenye Ulemavu Jenista Mhagama.
No comments:
Post a Comment