Shughuli za uoshaji wa Karoti zikiendelea kando ya mto Karanga,shuguli ambayo pia inatajwa kuwa chanzo cha uchafuzi wa mto huo ambao maji yake yanatumiwa na wakazi wa vijiji vya Chekereni,Mijongweni,Weurweru na Kiyungi wilaya ya Moshi vijijini.
Maeneo ambayo maji yenye kemikali kutoka viwandani yakiingia mto Karanga ,maji ambayo yanadaiwa kuwaathiri wakazi wa vijiji vya Chekereni,Mijongweni,Weruweru na Kiyungi wilayani Moshi vijijini.
Mmoja wa wakaz wa kijiji cha Chekereni akifua nguo kando ya mto Karanga ambao unaidaiwa maji yake yanawaathiri wakazi wa vijiji vilivyoko kando ya mto huo.
Na Dixon Busagaga wa globu ya jamii Moshi.
ZAIDI ya wakazi 1000 katika vijiji vya Chekereni, Mijongweni, Weruweru na Kiyungi wilayani Moshi vijijini inadaiwa wameathirika baada ya kutumia maji ya Mto Karanga yanayodaiwa kuwa na zinazotiririshwa kutoka kwa baadhi ya viwanda vilivyoko kando ya mto huo.
Mbali na athari hizo za kibinadamu pia mifugo inadaiwa kuathirika kutokana na kunywa maji hayo ambayo wakazi wa maeneo hayo wamekuwa wakiyatumia kwa shughuli za kufulia, kuogea na kunyweshea mifugo hasa kipindi cha kiangazi.
Uchunguzi uliofanywa katika mto huo umebaini mbali na kemikali hizo ambazo zimekuwa zikitiririshwa kwa wingi toka katika viwanda hivyo, pia shughuli za kilimo zinazoendelea pamoja na ujenzi ambao haukuzingatia sheria za mazingira zinachangia uchafuzi wa mto huo.
Shughuli nyingine ambazo zinachangia uchafuzi wa mto huo ni pamoja na wakulima wa karoti ambao wamekuwa wakiendelea na shughuli za kuosha zao hilo jirani kabisa na daraja la Bonite kabla ya kusafirishwa kwenda kwenye masoko ya ndani na nje ya mkoa wa Kilimanjaro.
Wakizungumza na waandishi wa habari ,Azama Ally mkazi wa kijiji cha Weruweru na Lusia Lucas mkazi wa kijiji cha Mijengweni wamesema maji hayo yamewaathiri kwa kupatwa na magonjwa ya upele,kukohoa kutokana na kuvuta hewa sanjari na kuumwa Macho kutokana na kutumia maji hayo kwa kufulia na kuogea.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kitongoji cha Bombani katika kijiji cha Chekereni/Werurweru, Leonard Munishi, amekiri kuwepo kwa hali hiyo huku akisema uchafuzi wa mazingira katika eneo hilo ni wa hali ya juu na kwamba wamebaini kuwa kemikali hizo zinatoka katika viwanda vilivyoko kando ya mto huo.
Naye Mwenyekiti wa Kitongoji cha Relini, Sadick Kubingwa, amesema kwa zaidi ya miaka 15 sasa maji hayo yamekuwa yakitiririka katika mto huo na kwamba yamechangia pia kwa kiwango kikubwa kuwepo kwa magonjwa ya milipuko katika vijiji hivyo.
No comments:
Post a Comment