Wajumbe wa Baraza kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa walipokutana siku ya jumatatu kujadili hali ya Usalama katika Kanda ya Afrika ya Sahel ambapo pia walijadili mapinduzi ya kijeshi nchini Mali na kutoka na taarifa iliyolaani mapinduzi hayo na kuwataka wanajeshi kurejea makambini na kurejesha utaratibu wa katiba pamoja na kufanyika kwa uchaguzi kama ilivyopangwa.
Rais wa Baraza Kuu la Usalama kwa mwezi wa Machi, Balozi wa Uingereza katika Umoja wa Mataifa, Bw. Mark Lyall Grant akifafanua jambo mara baada ya kukamilika kwa mkutano wa Baraza hilo ambalo pamoja na kulaani mapinduzi ya kijeshi nchini Mali, pia lilielezea hali tete ya kukidhiri kwa ukame, uhaba mkubwa wa chakula, kuongezeka kwa makundi yenye silaha, ugaidi na kusambaa kwa silaha katika eneo la kanda ya Sahel hali inayotishia siyo tu usalama wa eneo hilo, bali imesababisha pia mamia ya wananchi kukimbilia nchi jirani kutafuta misaada ya kibinadamu. Katika kikao hicho, Baraza hilo limezitaka jumuia ya kimataifa yakiwamo mashirika ya kimataifa kuharakisha misaada ya kibinadamu katika eneo hilo.
Na Mwandishi Maalum - New York
Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, limelaani vikali mapinduzi ya kijeshi yaliyofanywa na askari wa chache dhidi ya serikali ya kidemokrasia nchini Mali. Na limewataka wanajeshi hao kuachana na vitendo vya kihalifu na fujo na kurejea katika makambi yao
Taarifa iliyotolewa na Rais wa Baraza hilo kwa mwezi huu wa Marchi Balozi wa Uingereza Bw. Mark Lyall Grant amesema. “ Baraza la Usalama linalaani mapinduzi hayo na linawataka wanajeshi kurudi katika makambi yao na linatoa wito wa kurejeshwa kwa utaratibu wa Katiba na kufanyika kwa uchaguzi kama ilivyokuwa imepangwa.
Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa lilikutana siku ya jumatatu ambapo lilijadili kuhusu kuzorota kwa hali ya kibinadamu katika Kanda ya Afrika ya Sahel, ambapo lilisema kwamba kuongezeka kwa makundi yenye silaha na magaidi pamoja na kuzagaa kwa silaha kumeongeza hali ya wasiwasi katika kanda hiyo.
Wiki iliyopita baadhi ya wanajeshi wa nchi Mali wakiongozwa Kapteni Amadou Haya Sanogo walitangaza kuipindua serikali ya Rais Amadou Toumani Toure ambaye mpaka sasa hajulikano aliko.
Katika mkutano huo ambao uliwahusisha wajumbe 15 wanaounda Baraza Kuu la Usalama, Baraza hilo pia limelaani vitendo vinavyofanywa na baadhi ya makundi ya waasi ya kuvivamia vikosi vya serikali na kuwataka waasi hao kusitisha aina zote za vurugu na kutafuta ufumbuzi wa amani kwa njia ya mazungumzo ya kisiasa.
Aidha Baraza hilo limesisitiza haja ya kuzingatia na kuheshimu uhuru, umoja na mipaka ya nchi.
Tayari Umoja wa Afrika ( AU) umekwisha kutanga kutoyatambua mapinduzi hayo, huku baadhi ya nchi ikiwamo Marekani ikitangaza kusudio la kusitisha misaada kw anchi hiyo , nchi ambayo uchumi wake kwa asilimia kubwa unategemea sana misaada kutoka nchi wahisani
Kuhusu hali tete ya kanda ya Sahel, Baraza limebainisha kuwa hali ya ukame , uhaba wa chakula na kurudi kwa maelfu ya watu kutoka Libya kumeongeza hali ugumu wa maisha kwa watu wa eneo hilo. Hali ambayo imesababisha maelfu ya wananchi wa eneo hilo kukimbilia katika nchi za jirani kutafuta hali bora ya maisha.
Kutokana na hali hiyo, Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, limetoa wito kwa mamlaka za kitaifa na kimataifa, kikanda na masharika ya misaada ya kibinadamu kuchukua hatua za haraka kuimarisha juhudi za kuwasaidia wananchi wa eneo hilo.
Wanafiki wakubwa! Au inaonekana kuwa huenda wamepindua wanajeshi bila ya ubarakala wa nchi zenu za magharibi!
ReplyDelete