Shirika la Madini la Taifa ( STAMICO) katika muendelezo wa kuhakikisha linaendelea kuwa kinara katika kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi Tanzania nzima, leo tarehe 11/8/2026 imeingia mkataba mnono wa pande tatu kati ya STAMICO, Chuo cha Mafunzo na taasisi ya FDH ya kuhakikisha magereza yote ya Zanzibar yanaanza kutumia Nishati ya Rafiki Briquettes.
Makubaliano hayo yamefanyika katika ukumbi wa Chuo cha Mafunzo Zanzibar na kushuhudiwa na Kamishna wa Magereza Zanzibar Khamis Abdalah Khamis pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt Venance Mwasse na Mkurugenzi wa FDH Bwn Michael Salali.
Akiongea katika hafla hiyo, Dkt Mwasse ameipongeza taasisi ya FDH kwa kufanikisha kuingia makubaliano haya ambayo yatawezesha Magereza zote za Zanzibar kupata Nishati hii ya Rafiki Briquettes ambayo inaenda kuleta afueni kwenye gharama za Nishati kwa Magereza lakini pia kuanza kutekeleza agenda ya Nishati Safi kwa taasisi zote zinazohudumia watu zaidi ya 100.
"Suala la Nishati Safi ni Agenda ya Kitaifa na sisi STAMICO tumeibeba kwa mikono miwili kuhakikisha tunatumia Nishati yetu ya Rafiki Briquettes kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi" amesema Dkt Mwasse
Dkt Mwasse pia ameahidi kusaidia kuleta mafunzo na Kongamano la kuhamasisha matumizi ya Nishati Nzima kwa Watumishi wa Magereza na Wananchi wote wa Zanzibar.
Awali akiongea na kutoa salamu kutoka FDH, Bwn Salali ameahidi kuhakikisha taasisi yake kwa kushirikiana na STAMICO itahakikisha Nishati hii inafika kwenye Magereza yote kwa wingi na inafika katika ubora unaostahili.
Naye, Kamishna Khamis ameishukuru na kuipongeza STAMICO kwa kuhakikisha Nishati hii inafika Zanzibar.
Ameomba pia STAMICO iangalie kuwapa fursa hii ya kusambaza Nishati hii kwa wale wafungwa ambao wamemaliza vifungo vyao ili iwe njia ya kujitengenezea Kipato baada ya kumaliza vifungo vyao.
Kamishna ametoa rai kwa taasisi nyingine kuhakikisha ziznaanza kutumia Nishati Safi kuendana na agenda ya kitaifa ya Nishati Safi ili kulinda mazingira.
Naye, Mwenyekiti wa Wanawake na Samia Bi Fatuma Madidi ameipongeza STAMICO kwa juhudi za kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi na akapigia msumari kwenye suala la kuhakikisha na taasisi yake hiyo inashiriki kikamilifu kuisambaza Nishati ya Rafiki Briquettes katika kona zote za Tanzania.
STAMICO imejipanga kuhakikisha inaendelea kuwa kinara katika kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi Tanzania Nzima.





No comments:
Post a Comment