HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, May 25, 2026

Zawadi Ligi ya Muungano Kuboreshwa

 Na; Mwandishi Wetu, Unguja

WAZIRI  wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema msimu ujao wa Ligi ya Muungano utaboreshwa zaidi ikiwa pamoja na zawadi kwa bingwa ili kuipa hadhi ya kipekee ligi hiyo.

Amesema lengo ni kuifanya ligi hiyo inakuwa moja ya ligi bora Afrika Mashariki na kuifanya kuwa na mvuto wa aina yake kwa wapenda soka akieleza kuwa michezo ndio sehemu ambayo jamii hukutana na kuongea lugha moja.

Mhe. Masauni ameyasema hayo Mei, 24, 2026 Unguja, Zanzibar wakati wa halfa ya utoaji tuzo na zawadi kwa walioshiriki na kufanikisha Ligi ya Muungano 2026 ambapo Simba ilitawazwa mabingwa kwa kuifunga Yanga bao 1-0 katika mchezo uliochezwa Uwanja wa Amaan Complex.

“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar zimeendelea kuchukua hatua madhubuti za kuimarisha Muungano kwa misingi ya Kikatiba, Kihistoria, Mshikamano wa Kitaifa na maendeleo ya pamoja.

“Juhudi hizo zinajielekeza kuhakikisha kuwa jamii ya Watanzania inakuwa na umoja na ushirikiano katika nyanja zote za kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Mhe. Masauni amesema, Ofisi ya Makamu wa Rais ambayo ndiyo yenye dhamana na masuala ya Muungano kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kuwa sehemu ya uratibu wa Ligi ya Muungano ili kuongeza nguvu.

Amesema hatua hii itasaidia kuboresha maandalizi ya ligi ikiwemo kuboresha zawadi kwa washiriki na mshindi wa ligi.

“Nizipongeze timu zote ambazo zilishiriki mashindano haya kwa mwaka 2026 maana ushiriki wao ndio mafanikio ya uwepo wa Ligi hii ya Muungano.”

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Dkt. Riziki Pembe Juma amesema pamoja na ligi hiyo kusimama kwa muda mrefu lakini ilipotangazwa kurejea wadau waliitikia vizuri na kutoa ushirikiano.

“Awali kama wizara tulianza kwa wasiwasi lakini mwisho tulimaliza kwa furaha kwani tumegundua michezo imekuwa kitu cha kipekee na tutazidi kushirikiana na kumalizika kwa msimu huu inafanya tuanze maandalizi kwa ajili ya mwaka ujao,” amesema Mhe. Dkt. Riziki.

Naye, Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFF), Hussein Ahmada amezishukuru serikali za pande zote mbili kwa kuifanya michezo kuwa moja ya eneo la kuwaunganisha Watanzania kupitia Ligi ya Muungano akieleza kuwa hali hiyo imekuwa faraja kwa wapenda soka kuona nao wanathaminiwa.

Mwaka huu ligi hiyo ilishirikisha timu nane ambazo ni Simba iliyotwaa ubingwa, Yanga, Azam na Singida Black Stars kutoka Tanzania Bara wakati kwa Zanzibar ilikuwa Mlandege, KVZ, Mafunzo na Muembe Makumbi.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad