Akisoma maelezo ya awali ya shtaka hilo mbele ya Hakimu Mkazi Mhe. Lukosi, Mwendesha Mashtaka wa Serikali Wakili Nicas Kihembe akisaidiana na Erick alidai kuwa washtakiwa hao walikamatwa tarehe 08 Desemba 2025 katika mtaa wa Wailes, Temeke, Dar es Salaam, na maofisa wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), wakihusishwa na usafirishaji wa dawa za kulevya.
Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, wakati wa operesheni hiyo, DCEA ilikamata pakiti 20 za Bangi aina ya skanka zenye uzito wa jumla wa kilogramu 20.03, ambazo zilikuwa zimefichwa ndani ya balo la mitumba, kisha kufichwa katika basi aina ya Scania la kampuni ya King Masai Tours, lenye namba za usajili wa Msumbiji AAM 297 CA.
Ilielezwa zaidi kuwa, mashtaka yanayowakabili washtakiwa ni kosa la jinai chini ya kifungu cha 16(I) cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, inayokataza umiliki, usafirishaji na biashara ya dawa za kulevya nchini.
Upande wa mashtaka uliieleza mahakama kuwa, shtaka hilo halina dhamana kutokana na uzito wa dawa za kulevya walizokutwa nazo washtakiwa
Aidha, kwa mujibu wa wakili wa Serikali, upelelezi wa shauri hilo namba 1535/2026 ya mwaka 2026 bado unaendelea na mashahidi wanatarajiwa kufikishwa mahakamani hapo siku itakayopangwa.
Shauri hili lilihairishwa hadi tarehe 05 februari 2026, huku washtakiwa wakirejeshwa rumande.








No comments:
Post a Comment