NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Patrobas Katambi (Mb), ametoa wito kwa wananchi na mamlaka zote zinazohusika kudhibiti mianya isiyo rasmi inayoruhusu kuingizwa kwa bidhaa zisizo na viwango nchini.
Ameyasema hayo katika ziara yake kwenye Makao Makuu ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS) Desemba 20,2025 ambapo Mhe.Katambi amewahimiza Watanzania kuendelea kutumia huduma za Shirika hilo.
Pia amewatahadharisha wafanyabiashara kuepuka kuisababishia Serikali hasara kwa kukwepa kodi au kuingiza bidhaa duni zinazoweza kuhatarisha afya za wananchi, ikiwemo kusababisha magonjwa hatarishi kama saratani.
Mhe. Katambi amesema TBS iko tayari kutoa huduma kwa wafanyabiashara kwa kupokea sampuli za bidhaa na kuzifanyia tathmini ili kuthibitisha ubora wake, hatua ambayo huipa bidhaa uhalali na uhai sokoni.
Aidha ameitaka jamii kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na TBS kwa kutoa taarifa ili kuhakikisha kila bidhaa inayoingia nchini inapitia ukaguzi wa viwango.
Katika masuala ya vipimo na nishati, Mhe. Katambi amesisitiza umuhimu wa kuzingatia ubora wa vifaa vya umeme, ikiwemo matumizi ya taa zenye viwango vinavyokubalika, sambamba na juhudi za kitaifa za kuhimiza matumizi sahihi ya nishati.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt. Ashura Katunzi, amesema viwango vya kitaifa vinavyotolewa na TBS hutengenezwa kwa kushirikisha wadau husika katika kila sekta na kueleza kuwa TBS ina maabara nane zinazotambulika kimataifa na wataalam wake hutumika pia katika nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kufanya tathmini na ukaguzi.
Amebainisha kuwa TBS imeshiriki pia katika miradi mikubwa ya kimkakati kama ujenzi wa reli ya kisasa (SGR), Bwawa la Mwalimu Nyerere na miradi ya flyover, kwa lengo la kuhakikisha vifaa vinavyotumika vina ubora unaotakiwa.
Saturday, December 20, 2025
Home
Unlabelled
NAIBU WAZIRI KATAMBI ATEMBELEA OFISI ZA TBS, AFURAHISHWA NA UTENDAJI KAZI
NAIBU WAZIRI KATAMBI ATEMBELEA OFISI ZA TBS, AFURAHISHWA NA UTENDAJI KAZI
Subscribe to:
Post Comments (Atom)



























No comments:
Post a Comment