KUNDI la Majadiliano la Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (AGN)limeweka msisitizo katika dhamira yake ya kuhakikisha Afrika inazungumza kwa sauti moja imara katika majadiliano ya kimataifa kuhusu hali ya mabadiiko ya tabia ya nchii na madhara yake.
Mwenyekiti wa kundi hilo, Dk Richard Muyungi kutoka Tanzania, alisisitiza umuhimu wa kuendelea kupatiwa msaada wa kisiasa, kitaalamu na kifedha ili kusaidia nchi za Afrika kukabiliana na changamoto zinazotokana na mabadiliko ya tabia ya nchi pamoja na uwakilishi bora katika jukwaa la kimataifa.
Akizungumza wakati wa maadhimisho ya miaka 30 ya AGN yaliyofanyika pembezoni mwa Mkutano wa COP30 mjini Belém, Brazil jana, Dk Muyungi, ambaye pia ni Mjumbe Maalum na Mshauri wa Rais kuhusu Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi, alisema kundi hilo litaendelea kulinda maslahi ya Afrika katika masuala ya tabianchi.
“AGN itaendelea kulinda maslahi ya Afrika ili kupunguza athari zinazotokana na mabadiliko ya tabia ya nchi ambazo zinaathiri maeneo mbali mbali ikiwemo afya, kilimo na mengine mengi," alisisitiza Dk Muyungi.


No comments:
Post a Comment