MGOMBEA wa nafasi ya Rais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa amani ya nchi ndiyo hoja ya kwanza na ya msingi ya Chama Cha Mapinduzi, akisisitiza kuwa maendeleo hayawezi kupatikana bila kudumisha amani na umoja wa wananchi.
Akihutubia mamia ya wanachama wa CCM na wananchi katika mkutano wa kampeni uliofanyika Uwanja wa Michezo wa Msuka, Jimbo la Konde, Mkoa wa Kaskazini Pemba, Dkt. Mwinyi alisema wananchi wana wajibu wa kuilinda amani iliyopo kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.
Mkutano huo ulihudhuriwa na makundi mbalimbali ya wananchi wakiwemo wavuvi, wajasiriamali, mama lishe, waendesha bodaboda, akinamama na wajane.
Aidha, Dkt. Mwinyi amesema kuwa CCM inajivunia mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kuimarisha umoja na maridhiano ya Wazanzibari, jambo lililowezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo Unguja na Pemba.
Akigusia sekta ya elimu, Rais Dkt. Mwinyi alisema ongezeko la ufaulu wa wanafunzi ni ishara ya mafanikio katika sekta hiyo, huku akiahidi ujenzi wa skuli za kisasa zaidi katika maeneo mbalimbali ya visiwa hivyo.
Halikadhalika, Dkt.Mwinyi amebainisha kuwa Serikali iko katika hatua za mwisho za kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama, na kuhakikisha ukamilishaji wa ujenzi wa Bandari za Wete na Shumba ili kuongeza ufanisi katika usafirishaji wa mizigo na abiria.
Kuhusu miundombinu ya barabara, Dkt. Mwinyi amesema Serikali imejipanga kukamilisha ujenzi wa barabara kuu na zile za ndani katika muda mfupi ujao, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kuboresha huduma za kijamii na kiuchumi kwa wananchi.
Vilevile, ameahidi kuwa katika awamu ijayo Serikali itaongeza pensheni kwa wazee na wastaafu, pamoja na kuwawezesha wanawake wanaojishughulisha na kilimo cha mwani kwa kuwapatia mikopo isiyo na riba na boti kwa wavuvi.
Akizungumzia gharama za maisha, Dkt. Mwinyi amesema kupanda kwa bei za vyakula kumesababishwa na gharama za usafiri, na kwamba Serikali imechukua hatua ya kuimarisha bandari ikiwemo ya Mkoani, ili kupunguza gharama za usafirishaji na kushusha bei za bidhaa sokoni.
Dk.Mwinyi ameeleza kuwa Serikali inaendelea na ujenzi wa maghala ya kuhifadhia chakula, na itanunua mazao kutoka Tanzania Bara wakati wa mavuno kwa lengo la kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha kutosha na kudhibiti bei.
Kuhusu zao la karafuu, Dkt. Mwinyi amesema Serikali imeamua kuwakabidhi wananchi hati za mashamba ya Serikali ili wayatunze na kuongeza uzalishaji, huku akiahidi kuendeleza juhudi za kuliimarisha zao hilo kuwa nguzo kuu ya uchumi wa Zanzibar.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Dkt. Muhammed Said Dimwa, amesema Serikali imefanya maendeleo makubwa katika Mkoa wa Kaskazini Pemba, na wananchi wana kila sababu ya kumchagua tena Dkt. Mwinyi kwa kuwa ni kiongozi mkweli, muadilifu na mwenye kutimiza ahadi zake.
No comments:
Post a Comment