HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, August 16, 2025

TBL YAWEZESHA WAKULIMA WA SHAIRI MONDULI JUU KUHUSU UJUZI WA KUONGEZA NA KUBORESHA UZALISHAJI

Na Mwandishi Wetu,Monduli

TANZANIA Breweries Plc (TBL), mshiriki muhimu katika mnyororo wa thamani wa kilimo nchini Tanzania, imechukua hatua madhubuti kuimarisha kilimo cha shayiri nchini kwa kukutana na wakulima wa Monduli Juu, Arusha, na kuwapatia mafunzo ya vitendo na ushauri wa kitaalamu wenye lengo la kuongeza mavuno na kuboresha ubora wa zao.

Kikao hicho cha kubadilishana maarifa kimefanyika wakati wa Siku ya Wakulima wa Shayiri, hafla iliyoongozwa na viongozi wa serikali za mitaa na uwepo wa Katibu wa Wilaya ya Monduli Mkoani Arusha Muhsin Kassim.

Tukio hilo limewaleta pamoja wakulima 200, viongozi wa jamii, na wadau wa sekta ya kilimo kujadili suluhu za kufanikisha ukuaji endelevu wa uzalishaji wa shayiri.

Hafla hii ya kila mwaka imekuwa jukwaa la kutambua na kuthamini mchango wa wakulima hodari katika usambazaji wa shayiri nchini. Pia imesisitiza dhamira ya serikali kuendelea kuunga mkono sekta ya kilimo kama mhimili wa ukuaji wa uchumi, hasa katika mikoa kama Arusha ambako kilimo cha shayiri kimekuwa chanzo cha kipato na ajira kwa maelfu ya kaya.

Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Tawala wa Wilaya ya Monduli, Muhsin Kassim, amewaeleza wakulima kuhusu juhudi za serikali katika kuongeza tija, upatikanaji wa pembejeo, na upanuzi wa masoko ya shayiri na mazao mengine muhimu.

“Wakulima ndiyo uti wa mgongo wa taifa letu. Leo tunasherekea kazi zao na tunathibitisha upya dhamira yetu ya kuwasaidia kupitia utafiti, huduma bora za ugani, na upatikanaji wa masoko yenye tija,”alisema.

Tanzania Breweries Plc (TBL), mmoja wa wanunuzi wakubwa wa shayiri inayolimwa hapa nchini, ilishiriki katika hafla hiyo na kutoa shukrani kwa wakulima wanaowauzia zao hili muhimu, kwa kuwapa ujuzi wa kipekee utakaowasaidia kuboresha uzalishaji.

Shayiri ni malighafi ya msingi katika shughuli za utengenezaji wa bia wa TBL, na kwa miaka mingi kampuni imekuwa ikiunga mkono wakulima wadogo kupitia mikataba salama ya mauzo pamoja na mafunzo ya kilimo bora.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa masuala ya sheria na mahusiano ya kampuni ya TBL, Bi. Neema Temba amesisitiza msimamo wa kampuni kuendelea kununua mazao kutoka ndani ya nchi na kuwawezesha wananchi kupitia ushiriki shirikishi wa kiuchumi.

“Matukio kamahaya yanatukumbusha nafasi muhimu ya wakulima siyo tu katika usalama wa chakula, bali pia katika kuendeleza viwanda kama chetu. TBL tumejikita katika kuimarisha uhusiano na wakulima na kuunga mkono kilimo endelevu kinachowanufaisha wote katika mnyororo wa thamani,” alisema.

Hafla hiyo ilihusisha pia shamba darasa na vipindi vya kubadilishana maarifa. Pia ilitumika kama jukwaa la kujadili changamoto zinazokumba ekosistimu ya shayiri ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, upotevu wa mazao baada ya mavuno, na upatikanaji wa pembejeo bora, pamoja na kutafuta suluhu za pamoja kwa siku zijazo.

Siku ya Wakulima wa Shayiri ilihitimishwa kwa mwito wa pamoja kutoka kwa wadau wote wa sekta hii kuimarisha zaidi ushirikiano kati ya sekta binafsi, wakulima, na taasisi za serikali ili kuongeza tija, uendelevu, na upatikanaji wa masoko kwa wakulima katika mnyororo wa thamani wa shayiri.

TBL pia ni biashara endelevu iliyo na dhamira ya kuhamasisha na kuwawezesha wateja wake kujenga Dunia Bora. Hii ni kwa sababu kujenga dunia bora ni jukumu linalowezekana tu pale tunaposhirikiana, hata kama tupo mbali mbali.




No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad