Wasanii nyota wa muziki wa Bongo Fleva, Harmonize na Dulla Makabila, wanatarajiwa kutoa burudani kabambe katika mkesha wa Mwenge wa Uhuru utakaofanyika katika Viwanja vya Shule ya Msingi Makuburi, Wilaya ya Ubungo, tarehe 5 Juni 2025.
Burudani hiyo ni sehemu ya shamrashamra zitakazofanyika baada ya mbio za Mwenge wa Uhuru ambao unatarajiwa kupokelewa rasmi katika stendi ya Kibamba kuanzia saa 12:00 asubuhi, ukitokea Wilaya ya Kinondoni.
Mbali na burudani hiyo, mkesha wa Mwenge wa Uhuru utaambatana na utoaji wa elimu kuhusu Uchaguzi Mkuu wa 2025 pamoja na huduma za bure za afya ikiwemo upimaji wa virusi vya UKIMWI, malaria na magonjwa mengine.
Mwenge wa Uhuru utakimbizwa umbali wa takribani kilomita 72 ndani ya Wilaya ya Ubungo, ambapo utakagua, kutembelea na kuweka mawe ya msingi kwenye miradi 7 ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 8.2. Miradi hiyo inajumuisha sekta za elimu, afya, maji, barabara, maendeleo ya jamii, usafi na mazingira.
Aidha, mwenge huo utatumika kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 kupitia kaulimbiu isemayo “Jitokeze kushiriki Uchaguzi Mkuu 2025 kwa amani na utulivu.”
Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando, ametoa wito kwa wananchi wote kujitokeza kwa wingi kushiriki mapokezi ya mwenge, kukagua miradi, na kuhudhuria mkesha wa burudani kama ishara ya mshikamano na uzalendo.
No comments:
Post a Comment