HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, May 27, 2025

TCAA na Idara ya Uhamiaji Zatiliana Saini Mpango wa Kubadilishana Taarifa Kidijitali


Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) na Idara ya Uhamiaji wametiliana saini makubaliano ya mpango wa kubadilishana taarifa kwa njia ya kidijitali, hatua muhimu inayolenga kuimarisha usalama, kuongeza ufanisi wa huduma, na kusaidia ukusanyaji wa takwimu sahihi, hususan katika sekta ya utalii.

Makubaliano hayo yamesainiwa katika makao makuu ya Idara ya Uhamiaji jijini Dodoma kati ya Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Bw. Salim Msangi, na Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala.

Akizungumza katika hafla hiyo, Bw. Msangi alisema: “Mpango huu umekuja katika wakati muafaka ambapo dunia inazidi kukumbatia teknolojia ya kisasa. Utaongeza ufanisi wa operesheni zetu, kuimarisha usalama wa anga, na kusaidia udhibiti bora wa wageni wanaoingia na kutoka nchini kupitia viwanja vya ndege.”

Kwa upande wake, Kamishna Jenerali Makakala alieleza kuwa Idara ya Uhamiaji itaendelea kushirikiana kwa karibu na TCAA kuhakikisha taarifa za abiria na safari za anga zinawasilishwa kwa wakati na kwa usahihi.

“Huu ni muendelezo wa mashirikiano mazuri ambayo tayari yapo kati ya taasisi zetu. Tunaamini ushirikiano huu wa kidijitali utatuwezesha kuhudumia wananchi na wageni kwa weledi na haraka zaidi.”

Makubaliano haya pia yanatajwa kuwa chachu ya kuboresha ukusanyaji wa takwimu za wageni wanaoingia nchini, jambo litakalosaidia katika kupanga mikakati bora ya kukuza sekta ya utalii na uchumi kwa ujumla.

Hatua hii ni utekelezaji wa maelekezo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyesisitiza umuhimu wa taasisi za umma kushirikiana kwa karibu kupitia mifumo inayosomana ili kuongeza tija, kupunguza urasimu, na kuboresha huduma kwa wananchi.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Bw. Salim Msangi pamoja na Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala wakionesha mkataba wa makubaliano ya mpango wa kubadilishana taarifa kwa njia ya kidijitali hafla iliyofanyika katika makao makuu ya Idara ya Uhamiaji jijini Dodoma
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Bw. Salim Msangi pamoja na Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala wakisaini makubaliano ya mpango wa kubadilishana taarifa kwa njia ya kidijitali hafla iliyofanyika katika makao makuu ya Idara ya Uhamiaji jijini Dodoma
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Bw. Salim Msangi  akizungumza mara baada ya kusaini makubaliano ya mpango wa kubadilishana taarifa kwa njia ya kidijitali hafla iliyofanyika katika makao makuu ya Idara ya Uhamiaji jijini Dodoma
Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala akizungumza mara baada ya  kusaini makubaliano ya mpango wa kubadilishana taarifa kwa njia ya kidijitali hafla iliyofanyika katika makao makuu ya Idara ya Uhamiaji jijini Dodoma
Picha ya pamoja

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad