Abidjan. Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, leo, Mei 14, 2025, ameongoza mazungumzo ya kitaalamu kati ya Serikali ya Tanzania na Bw. Soren Toft, Afisa Mtendaji Mkuu wa Mediterranean Shipping Company (MSC), kuhusu uwekezaji wa kimkakati katika Bandari ya Dar es Salaam na Mangapwani–Zanzibar.
Mazungumzo hayo na kampuni ambayo makao yake makuu yapo Geneva, Uswisi, yamefanyika jijini Abidjan, Côte d’Ivoire pembezoni mwa Jukwaa la Maafisa Watendaji Wakuu Afrika, yakilenga fursa za kuboresha huduma na miundombinu ya bandari hizo mbili muhimu kwa uchumi wa taifa na ukanda wa Afrika Mashariki.
Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), kupitia kwa Mkurugenzi wa Fedha na Utawala, Bw. Pascal Maganga, kimeihakikishia MSC kuwa kipo tayari kushirikiana kikamilifu kwa kuhakikisha mazingira rafiki ya uwekezaji ili uwekezaji huo ufanyike kwa mafanikio makubwa.
Kwa upande wake, Bw.Toft ameonyesha dhamira ya dhati ya MSC kushirikiana na Tanzania katika kuimarisha miundombinu ya bandari, akisisitiza umuhimu wa Bandari ya Dar es Salaam na Mangapwani kama lango kuu la biashara kwa ukanda wa Afrika Mashariki.
Tanzania inaendelea kujidhihirisha kama kitovu cha uwekezaji barani Afrika, kwa kushirikiana na wadau wakubwa wa kimataifa katika kuendeleza miradi ya kimkakati itakayochochea uchumi wa nchi na ajira kwa wananchi.
No comments:
Post a Comment