NA BELINDA JOSEPH, RUVUMA.
Afisa Uhusiano na huduma kwa wateja kutoka TANESCO Mkoa wa Ruvuma Alan Njiro, amewataka wananchi kuingia mikataba ya makubaliano na mafundi wanaokuwa wakitekeleza ujenzi wa miundombinu ya umeme kwenye maeneo yote ya miradi pindi wanapohitaji kupata vitu mbalimbali kutoka kwao, ili kuhakikisha wanawalipa kabla ya kuikabidhi miradi kwa TANESCO.
Amesema kuwa mafundi hao hawaja ajiriwa na TANESCO wala wao hawawafahamu isipokuwa Mkandarasi aliechukua zabuni ya utekelezaji wa mradi, hivyo wasipokuwa makini na bidhaa wanazowakopesha watajikuta watu hao wanaondoka bila kuwalipa na hata watakapo kwenda kufuatilia TANESCO itakuwa vigumu kupata msaada, ikiwa mafundi hao hutoka maeneo mbalimbali ya nchi na wao watashindwa kuwatambua sababu hakuna mkataba wamauziano ya bidhaa baina yao na wananchi.
Ameyasema hayo wakati wa mwendelezo wa ziara yake ya utoaji elimu kwa wateja wa Shirika hilo, alipokita kambi Jimbo la Peramiho kuzungumza na wakazi wa Kata ya Maposeni na Peramiho kufuatia uwepo wa mradi wa REA ujazilizi hivyo amewataka kuhakikisha mikataba inakuwepo baina yao na mafundi ili kuepusha usumbufu.
Njiro ameeleza kuwa ni muhimu sana kama jamii kuwapa ushirikiano wakutosha mafundi katika kipindi chote ambacho mradi ukitekelezwa isipokuwa tu linapokuja swala lakuwakopesha pesa na vitu mbalimbali ndipo wahusishe mikataba ambayo itasaidia kulinda haki zao zisipotee.
Afisa Huduma kwa wateja Msaidizi kutoka TANESCO Ruvuma Bi Emma Ulendo, amewakumbusha wateja wapya wa shirika hilo kuwa malipo ya umeme hufanyika kwa njia ya namba ya kumbukumbu ya malipo na sio kumpa mtu mkononi hivyo ni muhimu zaidi kwenda wenyewe kulipia kupitia bank au mitandao ya simu ili kusaidia kutoibiwa na baadhi ya watu watakao watuma wakawasaidia kulipa na wasifikishe.
Diwani wa Kata ya Maposeni Monica Tambawa, amewapongeza TANESCO kuendelea kufikisha huduma kwa wakazi wa eneo hilo kwa kuongeza mradi wa REA ujazilizi, huku akiahidi kushirikiana na wananchi wote kuilinda miundombinu hiyo, pia ametumia jukwaa hilo kumpongeza Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Jenista Mhagama kuendelea kushirikiana na serikali kwa kuwasemea wananchi na huduma muhimu kuwafikia.
No comments:
Post a Comment