HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, April 16, 2024

SUA YAWAKUTANISHA MAAFISA WAANDAMIZI WA MAZINGIRA KUTOKA NCHI 10 ZA AFRIKA KUPITIA MRADI WA EFLOWS

 

 


Imebainishwa kuwa kuna umuhimu mkubwa wa kuwajengea uwezo watunga sera
hasa Makatibu Wakuu na Wabunge kuhusu athari za matumizi mabaya ya ardhi
katika maeneo ya vyanzo vya maji, Mito na kandokando ya Bahari ili kuwa na
uelewa wa pamoja wa athari hizo na mna ya kukabiliana nazo kwa manufaa ya
Taifa na vizazi vijavyo.

Wito huo umetolewa na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo
Prof. Raphael Chibunda wakati akifungua mafunzo ya siku saba kwa viongozi
waandamizi wanaosimamia masuala ya maji na mazingira kutoka nchi 10 za Afrika
zilizo kwenye ukanda wa Magharibi mwa Bahari ya Hindi yanayofanyika Jijini
Mbeya kupitia mradi wa Utafiti wa Usimamizi Endelevu wa Madakio ya Maji
Kupitia Tathmini ya Kuimarisha Mtiririko wa Maji kwa Mazingira na Utekelezaji
wake katika Kulinda Ukanda wa Magharibi mwa Bahari ya Hindi na Athari za
Shughuli za Kibinadamu Tanzania (EFLOWS).

“Pamoja na kazi kubwa ambayo nyinyi kama wataalamu mnaifanya mwisho wa
siku mtaandaa tarifa nzuri na kuwapelekea watunga sera ili waifanyie kazi, Lakini
bila wao kuelewa vizuri kwa kina mnayoandika baada ya kufanya tafiti mtajikuta
taarifa zenu mnazowaandikia hazifanyiwi kazi kama mnavyotegemea hivyo kuna
umuhimu mkubwa sana wa kujengeana uwezo nyinyi lakini pia kuwajengea
uwezo pia watunga sera maana ndio mnaowategemea katika kutelekeza yale
mnayowaplekea” Alifafanua Prof. Chibunda.

Amesema kuwa kuna tafiti nyingi sana zinafanyika kwenye nchi mbalimbali na
hata Tanzania ambazo zinalenga kutatua changamoto fulani lakini matokeo yake
hayaonekani moja kwa moja kwa jamii na Taifa kwakuwa wale wanaotegemewa
kuchukua matokeo hayo na kuyatumia pengine hawayatumii kwakuwa hawana
uelewa wa kina na wakutosha kuhusu yale ambayo tafiti zimebainisha.

Amepongeza kazi kubwa iliyofanywa na Watafiti kutoka SUA kwa kushirikiana na
Baraza la Taifa la Hifadhi ya mazingira NEMC katika utekelezaji wa Mradi wa
Tathimini ya maji kwa mazingira ambao matokeo yake mazuri ndio yamepekekea
Wataalamu hao kutoka nchi zote washiriki kuleta wataalamu wao kuja kujifunza
na kupanga mikakati ya pamoja na kukabiliana na changamoto hizo za
kimazingira.

Awali akieleza malengo ya mafunzo hayo Mtafiti Mkuu wa Mradi wa EFLOWS
ambaye pia ni Mkurugenzi wa Shahada za Uzamili, Utafiti, Uhauwilishaji wa
teknolojia na Ushauri wa Kitaalamu kutoka SUA Prof. Japhet Kashaigili amesema

utaalamu huo wa Tathimini ya maji kwa mazingira ambao umejengwa kupitia
mradi huo imeonekana ni muhimu sasa kuweza kuusambaza kwa wataalamu
kwenye nchi hizo ili kuwa na uelewa wa pamoja wa kukabiliana na changamoto
hizo za kimazingira.

“Mradi wa EFLOWS ambao tumeufanya kwa miaka miwili Wilayani Mbarali
Mkoani Mbeya na Wanging’ombe Mkoani Njombe ulikuwa mradi wa mfano
kuangali mtiririko wa maji na hali ya mto Mbarali matokeo yake yalilenga kupata
elimu ambayo itatumiwa na nchi zingine 10 za afrika, hivyo baada ya kukamilika
kwake sasa tumewaita wataalamu waandamizi kutoka nchi hizo kuja Tanzania
tujifunze na kubadilishana uzoefu kutokana na matokeo tuliyoyapata na kisha
kuja na maazimio ya pamoja ya namna ya kulinda ukanda wa magharibi mwa
Bahari ya Hindi kupitia mito na vyanzo vyake” alifafanua Prof. Kashaigili.

Aidha amesema kuwa changamoto nyingi za kimazingira zinazoonekana sasa
duniani ni matokeo ya shughuli za kibindamu ambazo zinagusa sekta mbalimbali
hivyo kutatua changamoto hizo ni lazima kuwe na jitihada za pamoja za kila mdau
kwenye sekta hizo na ndio maana wanawajengea uwezo kutambua na kuweka
mikakati ya pamoja ili kupata matokeo makubwa kwa wakati.

Kwa upande wake Wakili wa Serikali Mkuu kutoka ofisi ya Makamu wa Rais
Bwana Wankyo Mnono amesema mafunzo hayo ni muhimu kwa nchi zote
wanachama kwakuwa ulinzi wa Ikolojia ya Bahari ni muhimu kwa ustawi wa
viumbe na maisha ya watu maisha yao yanategemea rasilimali zinazopatikana
baharini.

“Tunatumia samaki na viumbe maji vingine kutoka Baharini na kwenye mito hivyo
swala la ulinzi wa ikolojia ya maisha ya samaki na viumbe vingine ni muhimu kwa
kuweka mipango na mikakati mizuri ya kuvilinda ili viendelee kutoa mchango kwa
jamii na taifa vizazi hadi vizazi lakini hilo litawezekana kama kutakuwa na
ushirikiano kwa nchi zote zilizo ukanda wa magharibi mwa bahari ya Hindi”
alieleza Bwana Wankyo.

Amesema kwa kutambua umuhimu wa kulinda Bahari na ikolojia yake Serikali ya
Tanzania inatarajia kutekeleza mradi mdogo wa utafiti utakaoangalia hali na
madhara ya matumizi ya mifuko na vifungashio vingine vya plastiki ili kupata
taarifa ambazo zitasaidia nchi kufanya maamuzi muhimu ya namna ya kukabiliana
na athari zinazotokana na matumzi ya plastiki kwenye bahari na nchi kavu.

Akitoa salamu kutoka Sekretarieti ya Azimio la Nairobi ambao ndio wafadhili wa
mradi huo Bwana Sammy Weru ameishukuru Serikali ya Tanzania na Chuo kikuu
cha Sokoine cha Kilimo kwa kuwezesha kufanyika kwa mafunzo hayo ya Kikanda
ambayo yana mchango mkubwa katika kulinda na kusimamia ukanda huo wa
bahari ya Hindi.

“Tunajisikia furaha kufanya kazi na SUA katika kutelekeza miradi mbalimbali
yenye tija kubwa kwa nchi zetu, na ninaamini kuwa kupitia mafunzo haya
tutatengeneza miongozo ya namna kusimamia masuala ya tathimini ya maji kwa
mazingira lakini bila kusahau kuzingatia dhana ya “kutoka Chanzo hadi baharini”
katika kuhakikisha usalama wa viumbe maji na ikolojia zao” alieleza Bwana Weru.

Mradi wa Utafiti wa Usimamizi Endelevu wa Madakio ya Maji Kupitia Tathmini ya
Kuimarisha Mtiririko wa Maji kwa Mazingira na Utekelezaji wake katika Kulinda
Ukanda wa Magharibi mwa Bahari ya Hindi na Athari za Shughuli za Kibinadamu
Tanzania (EFLOWS) unatekelezwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kwa
kushirikiana na Baraza la Taifa la hifadhi ya mazingira NEMC na wad au wengine
kwa ufadhili wa Sekretarieti ya Azimio la Nairobi.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael
Chibunda wakati akifungua mafunzo hayo jijini Mbeya.
Mtafiti Mkuu wa Mradi wa EFLOWS ambaye pia ni Mkurugenzi wa Shahada
za Uzamili, Utafiti, Uhauwilishaji wa teknolojia na Ushauri wa Kitaalamu
kutoka SUA Prof. Japhet Kashaigili akieleza malengo ya Mafunzo hayo yakimataifa.
Wakili wa Serikali Mkuu kutoka ofisi ya Makamu wa Rais Bwana Wankyo
Mnono akitoa salamu za Ofisi ya Makamu wa Raisi.
Muwakilishi wa Sekretarieti ya Azimio la Nairobi ambao ndio wafadhili wa
mradi huo Bwana Sammy Weru akitoa salamu kwa washiriki.
Prof. Denis Juizo Mkuu wa Kitivo cha Uhandisi kutoka Chuo Kikuu chaEduardo Mondlane cha Msumbiji akitoa neno la shukrani.
Picha ya Pamoja ya baadhi ya washiriki wa Mafunzo hayo pamoja na mgeni
rasmi Prof. Raphael Chibunda.


Picha za washiriki wa mafunzo hayo kutoka nchi kumi za
afrika wakifuatilia mafunzo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad