HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, April 17, 2023

KAMPENI YA UPANDAJI MITI YAWA KIVUTIO IFTAR YA NMB BUNGENI

 


NA MWANDISHI WETU, DODOMA


Kampeni ya Benki ya NMB ya kuongeza miti milioni moja katika ajenda ya serikali ya kuyatunza mazingira na kupambana na athari za tabia nchi imewakosha wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wakiongozwa na Spika Dkt Tulia Ackson, wawakilishi hao wa wananchi bungeni wameisifu taasisi hiyo kwa mradi huo mkubwa na wa kipekee nchini wengi wakisema ni wakizalendo na wenye manufaa makubwa kwa maendeleo ya taifa na maisha ya viumbe hai kwa ujumla.

Bunge limeahidi kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake na kuhakikisha kampeni hiyo ya kuikijanisha Tanzania inazaa matunda yaliyokusudiwa.

Wabunge hao walibainisha azma hiyo mwishoni mwa wiki jana baada ya kuvutiwa na uwekezaji huo na kuobwa na uongozi wa NMB kusaidia kuipeleka kampeni hiyo majimboni mwao.

Benki hiyo iliomba ushirikiano wa Bunge na wajumbe wake kwenye hafla ya Iftar ambayo iliiandaa Ijumaa bungeni ikiwa ni mwendelezo wa utamaduni wake wa kushirikiana na waumini wa dini ya Kiislamu kwenye Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

NMB imekuwa na utaratibu wa kuwafuturisha wadau na washirika wake likiwemo Bunge ambalo mara hii limetumia fursa hiyo kuipongeza taasisi hiyo kubwa ya fedha nchini kwa ukarimu huo na pia kuimwagia sifa kwa ushirki wake mkubwa katika ujenzi wa taifa na maendeleo ya Watanzania.


Mara baada ya futari hiyo ya kukata na shoka, Dkt Tulia aliipongeza NMB sio tu kwa kudumisha utamaduni wa kufuturisha bungeni, bali pia kwa kubuni kampeni endelevu ya upandaji miti na kuona umuhimu wa ushiriki wa wabunge kuifanikisha.

Kiongozi huyo alisema wameipokea kampeni hiyo iliyozinduliwa kitaifa Machi 27 na Makamu wa Rais, Dkt Philip Isidor Mpango, jijini Dodoma na kwa niaba ya wabunge wote kuahidi kuifanyia kazi.

Aidha, Dkt Tulia aliishukuru NMB kwa kutambua umuhimu wa kufanya ibada ya kufuturisha kwa kushirikisha wabunge, na kwamba kwa kufanya hivyo, benki inakuwa imeshirikisha wananchi wao, ambao wanawawakilisha bungeni.

"Sisi kama Bunge tumefurahishwa na mipango yenu yote iliyoelezwa na Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu , ambayo ni chanya na yenye manufaa makubwa kwa jamii na taifa kwa ujumla wake. Mipango hiyo ni muendelezo, kwani nina uhakika kila mbunge hapa jimboni kwake NMB imeacha alama kupitia uwajibikaji wake kwa jamii (CSR).

"Vitabu vyenu vya mapato vinaonesha mko vizuri na vinaakisi mchango mkubwa mnaoutoa kwa maendeleo ya taifa kutokana na kodi kubwa mnazolipa. Na kama haitoshi mnakuja na mipango muhimu kila uchao, ukiwemo huu wa upandaji miti milioni moja kote nchini mwaka huu,” alibainisha na kuongeza kuwa:

"Jambo hili ni la heri sana kwa ustawi wa mazingira yetu na kuwezesha vita ya kupunguza athari za mabadiliko ya tabia nchi. Nashukuru mmewataka wabunge kushirikiana nanyi kwa kuipeleka kampeni majimboni, nasi tunaahidi kufanya hivyo, tunaomba tu uwepo wepesi wa kutufikia kila tutakapowahitaji.”

Kwenye mahojiano baada ya kufuturu, baadhi ya wabunge, mbali na kuishukuru NMB kwa futari na kuisifu kwa ajenda yake ya kuchangia maendeleo endelevu, pia walisema benki hiyo ni kinara wa kulihudumia taifa kupitia ubunifu wa kidijitali na suluhisho za kifedha za viwango vya kimataifa.

Wabunge hao ambao ni pamoja na Mbunge wa Nyangwale, Bw Nassor Ammar, Mbunge wa Viti Maalujm, Bi Hawa Mchafu, na Mbunge wa Sengerema, Bw Hamis Tabasamu, walibainisha pia kuwa NMB inaongoza kwa kuwekeza katika miradi ya kijamii.

Aidha, walisema bajeti zake za CSR ni kubwa sana na ambazo ni mfano wa kuigwa kwa kusaidia kununua maelfu ya madawati kote nchini, kujenga madarasa na vyoo mashuleni, kuchangia vitanda mahospitalini, mashuka na vifaa vingine vya kuboresha utoaji wa huduma za afya.

NMB hutumia asilimia moja ya faida yake baada ya kodi kila mwaka kwa ajili ya kurudisha fadhila kwa jamii na kusaidia kutatua changamoto za wananchi, kiasi ambacho kwa mwaka huu, Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu Filbert Mponzi alisema kimeongezeka hadi TZS bilioni 6.2.

Akifafanua, Bw Mponzi alisema hii ni kutokana na Bodi ya Wakurugenzi kuidhinisha TZS bilioni 2 zaidi kwa ajili ya ajenda ya uendelevu yakiwemo masuala ya mazingira ambayo mradi wa kupanda miti milioni moja ni sehemu ya ufadhili huo mpya wa maendeleo endelevu wa NMB iliyopata faida ya TZS bilioni 429 mwaka 2022..

"Tumejipanga kupanda miti milioni moja kote nchini na hapa tutoe ombi kwa wabunge watusapoti kwa kupeleka kampeni hii katika maeneo yenu. Kwahiyo nawaomba wabunge wachangamkie fursa hii ili kuunga mkono jitihada za Serikali ya Rais Samia na Makamu wake Dkt Mpango za kuboresha na kuhifadhi mazingira," alibainisha

Afisa huyo mwandamizi pia akaeleza ya kuwa, yote hayo kwa mwaka huu yanaenda sambamba na sherehe zao za kutimiza miaka 25 ya kutoa huduma za kibenki nchini huku Bunge likichangia mafanikio makubwa waliyopata.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya NMB, Dkt Edwin Mhede, alitumia nafasi hiyo kuihakikishia Serikali na wanahisa wengine, kwamba pesa za hisa zao na mali ziko salama NMB, kwani wanajivunia uimara wa mtaji, thamani na faida wanayopata mwaka baada ya mwaka.

Spika wa Bunge ,Dk Tulia Ackson (katikati) akikaribishwa  na Mwenyekiti wa Bodi ya  Benki ya  NMB - Dk Edwin Mhede  (kulia) walipokutana kwenye hafla ya  futari iliyoandaliwa na benki ya NMB kwa Wabunge mwishoni wa wiki Bungeni Jijini Dodoma. kushoto ni  Afisa Mkuu  wa Wateja Binafsi  na Biashara wa benki ya NMB - Filbert Mponzi

Spika wa Bunge ,Dk Tulia Ackson (kulia) akikaribishwa na  Afisa Mkuu  wa Wateja wa Binafsi  na Biashara wa benki ya NMB - Filbert Mponzi (katikati) walipokutana kwenye hafla ya futari iliyoandaliwa na benki ya NMB kwaajili ya Wabunge mwishoni  wa wiki Bungeni Jijini Dodoma. kushoto kabisa ni Shekhe wa Mkoa wa Dodoma Shekhe Mstafa Rajabu.


Spika wa Bunge ,Dk Tulia Ackson (katikati) akizungumza na Mwenyekiti wa Bodi ya  NMB ,Dk Edwin Mhede pamoja na Afisa Mkuu  wa Wateja wa binafsi  benki ya NMB Makao makuu ,Filbert Mponzi walipokutana kwenye hafla ya  futari iliyoandaliwa na benki ya NMB kwa Wabunge mwisho wa wiki Bungeni Jijini Dodoma.



 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad