HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, January 14, 2023

BENKI YA CRDB KUSIMAMIA MFUKO WA FAIDA FUND UNAOENDESHWA NA WATUMISHI HOUSING

 
Dar es Salaam 14 Januari 2023 - WAZIRI wa nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora  Jenista Mhagama amezitaka taasisi zinazohusika na maendeleo ya vijana, wanawake na makundi maalum kuanza kuhamasisha makundi hayo  kuwekeza kwenye mfuko wa faida fund.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mfuko huo uliopo chini ya Watumishi Housing, Waziri Mhagama amesema Serikali isingependa kuona Watanzania wanaachwa nyuma katika shughuli za uwekezaji na ukuzaji wa mitaji.
Waziri huyo alitoa pongezi nyingi kwa shirika la uwekezaji katika makazi la Watumishi Housing kwa kuja na ubunifu huo ambao si tu  unatoa fursa ya wananchi kuwekeza kwa faida nzuri, bali pia unasaidia shirika hilo kupata mtaji wa utekelezaji wa miradi yake ya maendeleo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Watumishi Housing, Dkt. Fred Msemwa amesema uanzishwaji wa mfuko huo unatokana na maoni ya wawekezaji ambao wamekuwa wakipendelea kuwekeza mitaji yao kwa muda mfupi.

Dkt. Msemwa amesema pamoja na mafanikio makubwa ya mfuko wa awali wa uwekezaji katika sekta ya makazi (WHC-REIT) uliozinduliwa mwaka 2014 na kukusanya zaidi ya bilioni 59, baadhi ya wawekezaji hususan wawekezaji binafsi wamekuwa wakiomba kuanzishwa kwa mfuko utakaotoa fursa kwa wawekezaji wengi zaidi.
“Kwakuwa hili ni shirika la kizalendo tuliazimia kuyafanyia kazi maoni ya wawekezaji wetu. Leo hii tunajivunia kuzindua mfuko huu wa uwekezaji wa pamoja wa ‘FAIDA FUND’. Mfuko huu haubagui kiwango cha chini cha uwekezaji hivyo unatoa fursa Kwa mtanzania yoyote kujiunga,” alisema Dkt. Msemwa.

Mkurugenzi huyo wa Watumishi Housing aliwashukuru Benki ya CRDB ambao ni wasimamizi wa mfuko huo, pamoja na Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali, kampuni ya sharia ya Abenry Advocates, na Solomon Brokers kwa namna ambavyo wameshirikiana katika kuanzishwa kwa mfuko huo.
Akizungumza kwa niaba ya washirika wa mfuko huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Abdulmajid Nsekela aliishukuru Watumishi Housing kwa kuipa benki hiyo fursa ya kuwa msimamizi wa mfuko huo, na kubainisha kuwa benki hiyo imejipanga kuhakikisha Watanzania wote wanafiukiwa na kunufaika na fursa hiyo.

Akielezea faida ya mfuko huo, Nsekela amesema kuwa ni wa kipekee kwani umezingatia sera mahususi ya huduma jumuishi za kifedha zinazomjali Mtanzania wa rika zote ikiwa ni pamoja na kuweza kununua vipande kwa shilingi elfu 10 jambo ambalo linaenda sambaba na sera ya benki hiyo ya kuongeza ujumuishi wa kifedha.
 
Aidha amefafanua kwamba, mfuko wa faida fund unakuwa mfuko wa saba katika mifuko ya uwekezaji wa pamoja ambayo Benki ya CRDB. Hata hivyo amesema kuwa benki hiyo imejipanga kusimamia mfuko huo kikamilifu na kuhakikisha maslahi ya wawekezaji yanalindwa.
 Nsekela alimweleza Waziri Mhagama kuwa benki hiyo inajivunia kuwa kinara katika huduma bora za uwekezaji katika masoko ya mitaji.  Alibainisha kuwa Benki ya CRDB inachangia zaidi ya asilimia 70 ya wateja wote wanaoshiriki katika masoko ya mitaji na dhamana.

Mwaka jana Benki ya CRDB ilitunikiwa tuzo na Soko la Hisa la Dar es Salaam kwa kuitambua benki hiyo kama kinara wa huduma bora kwenye masoko ya mitaji. Benki ya CRDB ndio benki pekee nchini ambayo inatoa huduma ya kuuza na kununua bidhaa zote za masoko ya mitaji kupitia mtandao wa matawi yake kote nchini.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Jenista Mhagama (wanne kushoto) akiongoza zoezi la uzinduzi wa Mfuko wa Faida (Faida Fund), uliofanyika kwenye ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es salaam, Januari 14, 2023. Pamoja naye ni Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Damas Ndumbaro (watatu kushoto), Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba (wapili kulia) pamoja na viongozi wengine. Picha zote na Othman Michuzi
 
 Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mfuko wa Faida (Faida Fund), uliofanyika kwenye ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es salaam, Januari 14, 2023. 
 
 




No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad