HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, November 15, 2022

UBALOZI WA UFARANSA NCHINI WAZINDUA MAONESHO YA ELIMU YA JUU 2022


Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Nabil Hajlaoui akizungumza wakati wa uzinduzi wa Maonesho ya Elimu ya Juu kwa mwaka 2022 na kueleza kuwa kupitia fursa hiyo ya elimu nje ya Nchi vijana wa Tanzania watapata ujuzi ambao utasaidia katika masuala ya Teknlojia, Fizika, Sayansi pamoja na biashara.
Meneja Masoko wa Kitengo cha Afrika, Kituo cha Campus France Matthiew Bragato akizungumza wakati wa uzinduzi huo na kuwataka wanavyuo hao kutumia fursa hiyo ya kusoma nchini Ufaransa, na kuwatoa hofu kwa kuwaeleza kuwa masomo yanafundishwa kwa lugha ya kiingereza.


Baadhi ya wanavyuo wakipata mafunzo kutoka kwa wawakilishi wa vyuo vikuu saba kutoka nchini Ufaransa juu ya kunufaika na fursa ya kupata ujuzi kupitia vyuo vikuu vya Ufaransa, Leo Jijini Dar es Salaam.

 

USHIRIKIANO baina ya Tanzania na Ufaransa umeendelea kuimarika zaidi hasa katika sekta ya elimu ambapo Ufaransa kupitia Ubalozi wake nchini umezindua maonesho ya Elimu ya Juu kwa mwaka 2022 kwa vyuo vikuu 7 vya nchini Ufaransa kukutana na wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali vya Tanzania na kueleza program zinazotolewa katika vyuo vikuu vya Ufaransa kwa lugha ya Kiingereza.

 

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo uliofanyika katika kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC,) jijini Dar es Salaam Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Nabil Hajlaoui amesema kupitia fursa hiyo vijana wa Tanzania watapata ujuzi ambao utasaidia katika masuala ya Teknlojia, Fizika, Sayansi pamoja na biashara.

 

‘’Mje kama watanzania mkiwa mnazungumza Kiswahili na Kingereza mtapata ujuzi kwa lugha ya Kiingereza…Tunahitaji watanzania wengi kutoka vyuo vikuu vya Tanzania ambavyo tunashirikiana navyo kwa ukaribu zaidi na mkiwa Ufaransa mtafahamu pia tamaduni na lugha ya Kifaransa.’’ Amesema.

 

Balozi Nabil amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan alipokutana na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron walikubaliana kubadilishana ujuzi katika masuala ya Sayansi na Teknolojia ambapo kupitia fursa hizo za elimu katika kada mbalimbali zinazotolewa nchini Ufaransa ni moja ya nyenzo muhimu kwa vijana wa kitanzania katika kukuza Sayansi na Teknolojia nchini.

 

Aidha amesema kuwa wamekuwa wakishirikiana na vyuo vikuu vya Tanzania ili kujenga mahusiano mazuri  kwa pande zote mbili.

 

‘’Vijana wa Afrika wakiwemo wa hapa Tanzania wakitoka Ufaransa kupata mafunzo na ujuzi wamekuwa mstari katika nchi zao katika kusukuma gurudumu la maendeleo ya teknolojia na Nchi kwa ujumla tunawahimiza vijana wa Tanzania kuendelea kuchangamkia fursa hii.’’ Amesema.

 

Kwa upande wake Meneja Masoko wa Kitengo cha Afrika, Kitengo cha Campus France Matthiew Bragato amewataka wanafunzi hao kutumia fursa hiyo ya kusoma nchini Ufaransa, na kuwatoa hofu kwa kuwaeleza kuwa masomo yanafundishwa kwa lugha ya kiingereza.

 

‘’Tutumie fursa hii ili kuweza kubadilishana uzoefu wa Sayansi na Teknolojia kupitia elimu ambayo ujuzi unatolewa kwa lugha ya Kiingereza.’’ Amesema.

 

Bragato amesema, wawakilishi kutoka vyuo vikuu 7 kutoka nchini Ufaransa watawasilisha program bora zinazofundishwa kwa lugha ya Kiingereza na Kifaransa kwa wanafunzi wa vyuo Tanzania na  watakuwa nchini kwa kushirikiana na Kituo cha Campus France, Kiongozi wa Kifaransa wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Ufaransa anayeshughulikia uwezeshaji wa masomo nchini Ufaransa kwa wanafunzi wa kigeni.

 

Mkutano huo uliojikita katika mada mbalimbali ikiwemo masomo ya uhusiano wa kimataifa, masomo ya Kifaransa, masomo ya PhD, fursa za Erasmus Mundus na masomo ya biashara, pia jinsi ya kujiunga na kushiriki nafasi za masomo nchini Ufaransa pamoja na kujadili nafasi za kazi katika Nyanja hizo kwa nchi za Ufaransa na Tanzania.

 

Vyuo vikuu kutoka Ufaransa vilivyoshiriki na kuwasilisha program zao ni pamoja na Chuo Kikuu cha masomo ya kimataifa na siasa, shule tatu za uhandisi za IMT Ales, IMT Atlantique na ISEA- SUPAERO, shule mbili za biashara za Excelia na SKEMA pamoja na shule moja ya kilimo ya Institut Agro huku mamia ya wanavyuo kutoka Tanzania walitoka katika vyuo vilivyopo katika mikoa ya Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Morogoro, Iringa, Zanzibar na Mwanza.


Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Nabil Hajlaoui (Kulia,) akikagua maonesho hayo.


Mkutano ukiendelea.



Maonesho yakiendelea.
 


 
 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad