HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, November 10, 2022

TANZANIA, NORWAY KUIMARISHA USHIRIKIANO KATIKA KUPAMBANA NA MABADILIKO YA TABIANCHI

 WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Dkt. Selemani Jafo, katika vikao vya pembezoni mwa Mkutano wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi jijini Sharm El Sheikh nchini Misri, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Maendeleo ya Kimataifa wa Norway Bi Anne Tvinnereim katika banda la maonesho la Tanzania.


Katika mazungumzo hayo, mawaziri hao wamejadili na kukubaliana kuendeleza ushirikiano katika masuala ya maendeleo na hususan ufadhili katika miradi ya hifadhi ya mazingira na kuhimili mabadiliko ya tabianchi.

Dkt. Jafo amesema Serikali ya Tanzania na Norway zimekuwa na ushirikiano wa muda mrefu katika sekta mbalimbali na kusisitiza kuwa kwa sasa masuala ya mazingira yanazidi kupewa kipaumbe katika ushirikiano baina ya nchi hizo mbili.

Waziri Tvinnereim amesisitiza kuwa nchi ya Norway itaendelea kushirikiana na kufadhili miradi ya mabadiliko ya tabianchi nchini Tanzania kwa lengo la kusaidia wananchi walio katika hatari kubwa ya kuathiriwa na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Kwa upande wake Waziri Jafo alimshukuru Waziri Tvinnereim na Serikali ya Norway kwa ujumla kwa ushirikiano na misaada katika sekta mbalimbali za kiuchumi kwa Tanzania.

Alisema Tanzania iko tayari kushirikiana na Serikali ya Norway na kuendeleza ushirikiano huo kwa maslahi mapana ya nchi na maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Dkt. Jafo allisisitiza kuwa ajenda ya mabadiliko ya tabianchi ni changamoto kubwa duniani na inahitaji ushirikiano na ufadhili wa nchi zilizoendelea na zinazoendelea.

Tanzania ni mojawapo ya nchi zinazoshiriki mkutano huo unaofanyika Sharm El Sheikh nchini Misri kuanzia Oktoba 31 na kutarajiwa kuhitimishwa Novemba 18, 2022 ambapo Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan anaongoza Ujumbe wa Tanzania.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo akimkabidhi nyaraka mbalimbali Waziri wa Mambo ya Nje na Maendeleo ya Kimataifa wa Norway Bi Anne Veathe Tvinnereim katika banda la maonesho la Tanzania Sharm El-Sheikh, Misri leo tarehe 09/11/2022, mara baada ya kukamika kwa mazungumzo ya ushirikino baina yao.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Maendeleo ya Kimataifa wa Norway Bi Anne Veathe Tvinnereim katika banda la maonesho la Tanzania Sharm El-Sheikh, Misri. Mawaziri hao wametoa tamko la pamoja la kushirikiana katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

(PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad