HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, November 9, 2022

BENKI YA CRDB YAPONGEZWA JITIHADA ZA KUKUZA SEKTA YA UTALII ZANZIBAR

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,imesema itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Benki ya CRDB ili kuendelea kukuza uchumi.

Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale, Simai Mohammed Said, aliyasema hayo, katika ufunguzi wa warsha ya wadau wa sekta ya utalii na wateja wa Benki ya CRDB iliyofanyika katika ukumbi wa Golden Tulip Uwanja wa ndege.

Simai alisema Benki ya CRDB ina mchango mkubwa katika kuwezesha watalii kufanya miamala yao ya kifedha kwa urahisi na uharaka pindi wawapo nchini. Alisema uchumi wa Zanzibar kwa sehemu kubwa unategemea sekta ya utalii ambayo inakadiriwa kukua kwa asilimia 10 katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Akielezea mchango wa sekta ya utalii katika uchumi wa Zanzibar, Simai alisema, sekta hiyo inachangia karibu asilimia 80 ya fedha za kigeni visiwani humo na mchango wake kwenye pato la taifa ni asilimia 27.

Alisema, mchango wa ajira za moja kwa moja kutoka kwenye shughuli za utalii inatarajiwa kuongezeka kwa asilimia 50 katika miaka mitano ijayo,ambapo utalii huchukua asilimia 14.75 ya ajira zote za kulipwa Zanzibar na huajiri asilimia 60.6 ya wageni wote walioajiriwa Zanzibar.

Hivyo, alisema hatua hiyo imesababisha serikali iweke kipaombele kikubwa katika sekta hiyo kama ni moja ya sekta wezeshi katika kutekeleza dhana ya uchumi wa buluu.

Aidha alisema,viongozi wakuu wa Nchi, Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk.Hussein Ali Mwinyi,wamekuwa akihimiza kuboreshwa sekta ya utalii kama kitovu cha uchumi wa Zanzibar ambapo wamekuwa wakitangaza taifa kupitia filamu ya 'Royal Tour'.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Kadi wa benki ya CRDB Farid Seif alisema lengo la kuandaa semina hiyo ni kuwapa elimu juu ya huduma mbalimbali zinazotolewa naa benki hiyo ikiwamo huduma za malipo kupitia kadi na mifumo mingine, pamoja na uwezeshaji wa kibiashara kupitia  mikopo ya uendeshaji na uwekezaji.

Faridi alisema wamewapatia elimu wateja wao ili kukuza zaidi biashara zao sambamba na kupokea mapato kwa urahisi zaidi,ambapo benki hiyo imejiandaa kutoa huduma bora. Aidha alisisitiza kuwa benki yao itaendelea kushirikiana na serikali ili kuona uchumi wa nchi unakuwa sambamba na kukuza uchumi wa buluu hasa kupitia sekta ya utalii.

Nao wadau wa warsha hiyo wameishukuru Benki ya CRDB kwa kuandaa semina hiyo huku wakisema mifumo ya malipo ya benki hiyo imekuwa msaada mkubwa katika kuongeza ufanisi  katika utoaaji huduma kwa wateja wao ikiwamo watalii jambo ambalo piaa limesaidia katika ukusanyaji mapato katika biashara zao.

Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar, Simai Mohammed Said akizungumza na wadau wa sekta ya utalii wakati wa semina iliyoandaliwa na Benki ya CRDB kwa wadau wa sekta hiyo katika hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa ndege Zanzibar.
Mkuu wa Kitengo cha Kadi Benki ya CRDB,Farid Seif akizungumza na wadau wa sekta ya utalii wakati wa semina iliyoandaliwa na Benki ya CRDB kwa wadau wa sekta hiyo katika hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa ndege Zanzibar.
Meneja Mwandamizi wa Huduma za Malipo Benki ya CRDB, Victor Makere akitoa mada kuhusu huduma mbalimbali za malipo zinazotolewa na benki hiyo wakati wa semina iliyoandaliwa na Benki ya CRDB kwa wadau wa sekta ya utalii katika hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa ndege Zanzibar.
Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar, Simai Mohammed Said (wakwanza kulia) akizungumza Mkuu wa Kitengo cha Kadi Benki ya CRDB,Farid Seif (wakwanza kushoto) na wadau wengine wa sekta ya utalii wakati alipowasili katikansemina iliyoandaliwa na Benki ya CRDB kwa wadau wa sekta hiyo katika hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa ndege Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad