Na. James K. Mwanamyoto-Zanzibar
Tarehe 29 Oktoba, 2022
Mawaziri wenye dhamana ya kusimamia masuala ya utumishi wa umma na utawala bora wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jenista Mhagama na wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Haroun Suleiman wamefanya kikao kazi cha kujadili namna ya kuboresha utendaji kazi katika Utumishi wa Umma na Utawala Bora na kuweka msingi bora wa watumishi wa umma kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kuleta tija katika mandeleo ya taifa.
Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa kikao kazi hicho kilichofanyika Unguja Zanzibar, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na UtawalaBora, Mhe. Jenista Mhagama amesema kuwa, wamekubaliana kubadilishana maarifa na uzoefu kwa pande zote mbili za muungano katika eneo la utengenezaji wa mifumo ya TEHAMA ya usimamizi wa utendaji kazi na tathmini ya utendaji kazi kwa watumishi wa umma na taasisi za umma.
Mhe. Jenista amesema, kupitia kikao kazi hicho imesisitizwa uzingatiaji wa taratibu za ajira Serikalini, uzingatiaji wa maadili kwa viongozi na watumishi wa umma, usimamizi wa rasilimaliwatu, kuendeleza mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa, ikiwa ni pamoja vyuo vya utumishi wa umma kufanya tafiti zitakazosaidia kutoa mwongozo wa namna sekta ya utumishi wa umma nchini itakuwa na tija kwa maendeleo ya taifa.
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Afisi ya Rais Katiba Sheria Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Haroun Suleiman amesema kikao kazi hicho kimekuwa na faida kubwa katika kujenga ushirikiano wa kiutendaji kwenye masuala ya muungano na yasiyo ya muungano, kati ya ofisi yake na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora inayosimamiwa na Mhe. Jenista Mhagama.
Kutokana na uwepo wa ushirikiano huo kiutendaji, Mhe. Suleiman amesema kikao kazi hicho kimetoa tamko la kuwapongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa namna wanavyohimiza ushirikiano pamoja na kusimamia masuala ya utumishi wa umma na utawala bora.
Mhe. Suleiman ameongeza kuwa, anaamini kasi ya ushirikiano waliyonayo viongozi hao itaendelezwa pia na watumishi na watendaji walio chini yao, ili kufanikisha azma ya kuujenga utumishi wa umma na utawala bora wenye tija katika kutoa huduma bora kwa wananchi na kuleta maendeleo nchini.
Awali akisoma maazimio ya kikao kazi hicho, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi amesema kikao kimeazimia kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan na Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa uongozi wao katika kusimamia vizuri masuala ya utumishi wa umma na utawala bora.






Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama na Waziri wa Nchi, Afisi ya Rais Katiba Sheria Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Haroun Suleiman wakisaini masuala waliyokubaliana kuyatekeleza kupitia kikao kazi chao kilichojadili namna ya kuboresha utendaji kazi katika Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
No comments:
Post a Comment