HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, October 27, 2022

DIWANI SIRIA ATAKA MGOGORO WA MPAKA UTATULIWE

 DIWANI wa Kata ya Loiborsoit Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, Siria Baraka Kiduya ameitaka Halmashauri ya Wilaya hiyo kutatua mgogoro wa ardhi baina ya kata yake na kata ya Edonyongijape.


Kiduya ameyasema hayo kwenye kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya hiyo cha kujadili changamoto na mafanikio ya kata zao.

Amesema wananchi wa kata ya Loiborsoit wanasikitishwa ba kitendo cha baadhi ya wananchi wa kata ya Edonyongijape kulima mazao yao kwenye eneo la kata yao.

"Wataalam wa ardhi wanapaswa kutuonyesha mahali mpaka ulipo ili wananchi wetu wabaini na kufanya shughuli zao za maendeleo bila tatizo lolote," amesema Kiduya.

Diwani wa Kata ya Edonyongijape, Jacob Kimeso ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, amesema baadhi ya wataalam wa idara ya ardhi wamekuwa wakiwachangaya wananchi kwani wanakuja na ramani tofauti.

"Leo unawaambia wananchi mpaka wenu mwisho wake ni hapa kesho unawaambia mwisho ni kule hawataelewa zaidi ya kuwachanganya," amesema Kimeso.

Kwa upande wake Ofisa ardhi wa halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Baltazari Sulle amesema mpaka unaotambulika hadi hivi sasa ni ule wa mwaka 1991 Wilaya ya Simanjiro ikiwa ipo Wilaya ya Kiteto.

Sulle amesema Wizara ya Ardhi bado inatambua mpaka wa awali wa Loiborsoit na Edonyongijape kwani huo mwingine wa mwaka 2012 uliofanywa na mradi wa LAMP hautambuliki wizarani.


Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Baraka Kanunga amesema wataalam wa ardhi wanapaswa kuwashurikisha wananchi na viongozi husika ili kuepuka migogoro.

Diwani wa Kata ya Ruvu Remit Yohana Maitei Kadogoo amewataka viongozi kukubaliana na suala la mipaka kwani jambo la kuhofia kupoteza wapiga kura siyo lao ni Mungu anajua.
Diwani wa Kata ya Loiborsoit Siria Baraka Kiduya akizungumza kwenye kikao cha Baraza la Madiwani.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad