HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, September 5, 2022

SERIKALI YA AWAMU YA SITA YAKARABATI JENGO LA OFISI YA KARAKANA YA NDEGE ZA SERIKALI LILILOJENGWA MIAKA 65 ILIYOPITA

 Na. James K. Mwanamoto - Dar es Salaam

Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuboresha miundombinu ya utendaji kazi kwa kukamilisha ujenzi na ukarabati wa jengo la ofisi ya karakana ya ndege (HANGAR) la Wakala wa Ndege za Serikali (TGFA) ambalo lilijengwa na Serikali miaka 65 iliyopita.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (Mb) amesema, kukamilika kwa ujenzi wa karakana hiyo kunatokana na uongozi mzuri na jitihada za Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ambaye amejipambanua kwa vitendo kuwa ni kiongozi mwenye dhamira ya dhati ya kuleta maendeleo katika taifa letu.

Mhe. Jenista Mhagama amemshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa uongozi imara na jitihada za kuleta maendeleo kwa ustawi wa taifa na kuahidi kuunga mkono jitihada hizo kwa kusimamia vizuri miundombinu hiyo iliyoboreshwa na inayoendelea kuboreshwa kwa manufaa ya taifa.

“Awali nilikagua jengo lote, chumba kwa chumba, mlango kwa mlango, ili kujiridhisha na kiwango cha ujenzi kabla ya kuweka jiwe la msingi na kulizindua, hivyo ninauthibitishia umma kuwa nimelizindua jengo hili kwasababu limejengwa kwa ubora na viwango vinavyostahili,” Mhe. Jenista amefafanua.

Akitoa taarifa ya ujenzi wa jengo hilo la ofisi ya karakana ya ndege, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ndege za Serikali, Mhandisi John Nzulule amesema kuwa, kukamilika kwa jengo hilo kutasaidia kuboresha utekelezaji wa majukumu ya wakala kwa Idara zilizopo uwanja wa ndege kwani lina nafasi ya kutosha na mifumo ya kisasa itakayowawezesha Marubani, Wahandisi na Wahudumu wa ndege kutekeleza majukumu yao kikamilifu.

Naye, Kaimu Meneja Uhandisi wa Wakala wa Ndege za Serikali, Mhandisi Gratian Kyaruzi amesema ofisi ambazo wamekuwa wakizitumia ni chakavu, hivyo kukamilika kwa jengo hilo kumeboresha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi na kutaongeza ufanisi kiutendaji.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja Uendeshaji wa Wakala wa Ndege za Serikali, Bw. Budodi Nicholaus amemshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan na Msaidizi wake Mhe. Jenista Mhagama kwa kuwezesha kukamilika kwa ujenzi wa jengo hilo jipya la Ofisi ya Karakana ya Ndege za Serikali, ambalo litaboresha utendaji kazi katika eneo la usimamizi wa ndege ambazo zinazotoa huduma ya usafiri kwa viongozi wakuu wa kitaifa pindi wanapotekeleza majukumu yao.

Mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa jengo la ofisi ya karakana ya ndege (HANGAR), Serikali inaanza kutekeleza sehemu ya pili ya mradi huo kwa kujenga karakana ya ndege.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akikata utepe kuzindua jengo la ofisi ya Karakana ya Wakala wa Ndege za Serikali jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizindua jengo la ofisi ya Karakana ya Wakala wa Ndege za Serikali jijini Dar es Salaam.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad