HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 26, 2022

MKOA WA RUVUMA WAFIKIA ASILIMIA 63 YA LENGO LA KUHESABU KAYA 450,000

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Thomas Laban akizungumza na wananchi wa Mtaa wa Peramiho ambao tayari walikuwa wamehesabiwa katika zoezi la sensa ambalo linaendelea nchini kote 

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Laban Thomas alipowasili katika ofisi za Mtendaji Kata ya Peramiho Halmashauri ya Songea kwa ajili ya ukaguzi wa zoezi la sensa katika baadhi ya mitaa ya Kata hiyo
Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Laban Thomas akiwa na wajumbe wa Kamati ya Sensa Mkoa na Halmashauri ya Wilaya ya Songea akitembea katika baadhi ya mitaa kukagua mwenendo wa zoezi la sensa ambalo lilianza Agosti 23 na linatarajia kukamilika Agosti 28.

MKUU wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Laban Thomas amesema takwimu ya kitaifa ya sensa inaonesha kuwa hadi kufikia Agosti 26 mwaka huu saa moja asubuhi Mkoa wa Ruvuma ulikuwa umefikia asilimia 63 ya lengo la Kuhesabu zaidi ya kaya 450,000.

Kanali Thomas amesema hayo wakati anazungumza na wananchi wa Peramiho nje kidogo ya Mji wa Songea alipofanya ziara ya kukagua zoezi la sensa linaloendelea nchini kote.

Amesema kutokana na takwimu hizo za kitaifa Mkoa unakwenda vizuri ambapo ametoa rai kwa wananchi kuendelea kushirikiana na makarani kwa kujitokeza kuhesabiwa ili Mkoa uweze kupata takwimu za sensa za watu za kutosha ambazo zitaisaidia serikali kupanga mipango ya maendeleo.

Hata hivyo Kanali Thomas amesema anatamani Mkoa wa Ruvuma uvunje rekodi za kitaifa kwenye majumuisho ya sensa kwa kuongoza kitaifa.

RC Thomas amewapongeza watendaji kwa usimamizi mzuri katika zoezi la sensa ambapo amewataka viongozi wa Halmashauri zote kuendelea kuwaelimisha wananchi wajitokeze kuhesabiwa ili kufikia malengo ya Mkoa na taifa kwa ujumla

“Matumaini yangu tuakwenda vizuri niwaombe wananchi wenzangu endeleeni kujitokeza ili tupate data sahihi, data hizi zina manufaa kwetu na kwa taifa letu”alisema RC Thomas.

Naye Mkurugenzi wa Halmashaur ya Wilaya ya Songea Neema Maghembe ameeleza Halmashauri hiyo yenye Kata 16, inatarajia kuhesabu kaya zaidi ya 36,000, na kwamba hadi kufikia Agosti, 25, wameweza kuhesabu kaya zaidi ya 28,000.

“Nikuhakikishie Mkuu wa Mkoa zoezi hili linakwenda vizuri na watu wanajitokeza kuhesabiwa, hata kaya uliotembelea umekuta zoezi linakwenda vizuri” alisema Bi maghembe.

Mkoa wa Mkoa wa Ruvuma, anaendelea na ziara ya kukagua maendeleo ya zoezi la sensa ya watu na makazi katika Halmashauri za Mkoa wa Ruvuma.Zoezi hili lilianza Agosti, 23, 2022 na linatarajiwa kukamilika Agosti, 28 mwaka huu.

Imeandikwa na Albano Midelo

Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Mkoa wa Ruvuma

Agosti 26,2022

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad