HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, July 2, 2022

DKT. STERGOMENA ATEMBELEA MAONESHO YA SABASABA, ASHIRIKI MAADHIMISHO MIAKA 41 YA SUMAJKT

 






Waziri wa Ulinzi na JKT, Mheshimiwa Dkt. Stergomena Lawrence Tax (Mb) akiwa katika band la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMAJKT) lililopo katika maonesho ya ya 46 ya Kimataifa ya kibiashara yanayoendelea kufanyika katika viwanja vya sabasaba jijini Dar es Salaam.


WAZIRI wa Ulinzi na JKT, Mheshimiwa Dkt. Stergomena Lawrence Tax (Mb) ameshiriki Maadhimisho ya Miaka 41 ya Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMAJKT) yaliyofanyika katika Viwanja vya Maonyesho ya Sabasaba Temeke, Jijini Dar es Salaam.

Maadhimisho ya Miaka 41 ya SUMAJKT yanaenda sambamba na Maonyesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara kwa mwaka 2022 yenye Kaulimbu isemayo: Tanzania: Mahali Sahihi pa Biashara na Uwekezaji.

Katika Maadhimisho hayo, Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na JKT alipata fursa ya kutembelea, kujionea pamoja na kupata maelezo kuhusu bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na huduma zinazotolewa na Makampuni Tanzu chini ya SUMAJKT.

Akiongea na Waandishi wa Habari, Mheshimiwa Waziri amesema “naomba nianze kwa kutoa shukrani kwa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa kuandaa Maonyesho ya miaka 46 ya Biashara yenye Kaulimbiu isemayo Tanzania: Mahali Sahihi pa Biashara na Uwekezaji, sisi kama sehemu ya Maonyesho haya, sisi tunaadhimisha zaidi, kwa kusherehekea miaka 41 ya SUMAJKT”, alisema.

Aidha, Mheshimiwa Waziri ameongeza kusema “Maonesho haya yametupa fursa nasi kuja kufanya biashara, huku tukifanya Maonyesho ya kuadhimisha miaka 41 tangu kuanzishwa kwa SUMAJKT. Kama tulivyotembelea, tumejionea kuwa yapo mengi yamefanywa. Limekuwepo pia, swali linaloulizwa kuwa tunaposema Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania inamaanisha nini?, huu ni mfano mmojawapo. SUMAJKT Kama sehemu ya JWTZ imekuwa likitekeleza shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii kote nchini na kuchangia uchumi wa Taifa”, aliongeza.

Akitoa historaia ya kuanzishwa kwa SUMAJKT, Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa, Meja Jenerali Rajab Ndulu Mabele amesema “lengo la kuanzishwa kwa SUMAJKT ni kufanya biashara na kuzalisha faida ili kusaidia gharama za uendeshaji wa shughuli za JKT pamoja na kujenga uchumi wa Taifa”.

Jenerali Mabele ameongeza kuwa “ kwa hivi sasa SUMAJKT imeongezewa majukumu mengine ya kiuzalishaji ambayo yamekuwa yakichangia katika pato la Taifa. Tangu mwaka 2017 JKT imekuwa ikitoa gawio katika Mfuko Mkuu wa Serikali”, alisema.

Shirika hili linazalisha bidhaa na kutoa huduma bora kwa jamii katika sekta za kilimo, mifugo; sekta ya ujenzi; skta ya huduma za biashara na sekta ya viwanda. Vilevile, SUMAJKT linauza zana za kilimo ikiwemo Matrekta , mashine za kulimia na kupandi, pampu za kumwagilizia na vipuri vyake.

Adha, SUMAJKT tangu kuanzishwa kwake, kupitia viwanda na Kampuni yake Tanzu ya Ulinzi (SUMAJKT Guard Company Limited ) imeendelea kutoa mchango mkubwa kwa Taifa katika kupunguza tatizo la ajira nchini, ambapo Kampuni ya Ulinzi pekee imeweza kuajiri vijana zaidi ya 15,000, pia Kampuni ya Usafi (Cleaning and Fumigation Services) nayo ikiajiri vijana zaidi ya 1000.

SUMAJKT ni Shirika linaloendesha shughuli za uzalishaji mali ndani ya Jeshi la Kujenga Taifa. Shirika hili lilianzishwa rasmi tarehe 01 Julai, 1981 kwa Amri ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Sheria ya Uanzishaji wa Mashirika ya kibiashara katika Taasisi za Umma (The Corporation Sole Establishment) Act. No. 23 of 1974 (Cap 119 RE.2002).

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad