Afisa
Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna akimkabithi Mwenyekiti wa
Bodi ya Benki ya NMB, Dk. Edwin Mhede ripoti ya mwaka 2021 kwenye
Mkutano Mkuu wa 22 wa Wanahisa, uliofanyika ukumbi wa JNICC, Dar es
Salaam. Kushoto ni Afisa Mkuu wa Fedha wa NMB, Juma Kimori na Kaimu
katibu wa NMB, Consolatha Mosha. Afisa
Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna akizungumza kwenye Mkutano
Mkuu wa 22 wa Wanahisa, uliofanyika ukumbi wa JNICC, Dar es Salaam.
*******************
Wanahisa
wa Benki ya NMB wameidhinisha gawio la Sh 96.7 bilioni kwa mwaka 2021,
huku wakiwa na imani kubwa benki yao kuendelea kufanya vizuri zaidi
mwaka huu.
Gawio la mwaka 2021 linatokana na kuongezeka kwa faida
baada ya kodi kutoka Sh206 bilioni mwaka 2020 na kufikia Sh290 bilioni
mwaka jana, mwaka 2021
Katika Mkutano wake Mkuu wa 22 wa Mwaka
uliofanyika mwishoni mwa wiki, wanahisa walipitisha kiasi hicho cha
fedha ambacho ni sawa na malipo ya Sh193 kwa kila hisa kwa kipindi
kilichoishia Desemba 31, 2021 (wanahisa walipata gawio la Shs 137 kwa
kila hisa kwa mwaka 2020).
Akizungumza na wandishi wa habari,
Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB- Ruth Zaipuna alisema Benki hiyo
itaendeleza mwenendo wake wa kufanya vizuri kwa kuvuka malengo
iliyojiwekea kwa mwaka huu pia.
Matarajio hayo yanatokana na
matokeo mazuri ya robo ya kwanza ya mwaka huu ambapo Benki tayari
imepata faida baada ya kodi ya Sh101bilioni ikiwa ni ongezeko la
asilimia 55 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka jana.
“Ni
kweli tumeuanza mwaka 2022 vizuri. Mafanikio makubwa ya kiutendaji kwa
mwaka 2021 na matokeo mazuri ya robo ya kwanza ya mwaka 2022 ni
kielelezo cha ufanisi mzuri unaotokana na utekelezaji makini wa mikakati
yetu. Tutaendelea kutekeleza kwa umakini sana mikakati tuliyojiwekea na
tunaamini kwamba malengo tuliyojiwekea kama benki tutayafikia na
kuyapita mwaka huu wa 2022,” alisema Zaipuna.
Alisema kwa
mahesabu ya kawaida, matokeo ya robo ya kwanza ya mwaka huu yanaleta
picha kuwa utakuwa mwaka mzuri pamoja na changamoto zinazoendelea
kujitokeza duniani. “Kadri tunavyoendelea kukabiliana na mazingira ya
biashara yanayobadilika kwa kiasi kikubwa, tumejipanga kwa umakini
kupata matokeo mengine mazuri yatakayoendeleza rekodi yetu sokoni”
alisema.
Mwaka jana, Benki ya NMB ilifanikiwa kuvuka malengo yake
katika vigezo karibu vyote vya kiutendaji, huku amana za wateja
zikipanda hadi Sh6.6 trilioni na mikopo ikifikia Sh4.8 trilioni.
Benki
hiyo pia imeweka rekodi katika sekta ya benki kwa kuwa na uwiano bora
wa gharama za mapato wa asilimia 46 hadi kufika Desemba 31, 2021 ikiwa
imepungua kwa asilimia 5 ikilinganishwa na mwaka 2020 (asilimia 51),
huku uwiano wa mikopo chechefu (NPL) ukifikia asilimia 4 ya mikopo
ghafi, kiwango ambacho ni chini ya kile kinachotakiwa na Mdhibiti (Benki
Kuu).
Kwa ujumla katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita benki
ya NMB ilishuhudia Mizania bora, ukwasi wa kutosha na viwango thabiti
vya mtaji ambavyo viko juu ya viwango vya udhibiti. Benki hiyo pia
ilitambulika kimataifa kama benki bora na salama.
Mwenyekiti wa
Bodi ya Benki ya NMB, Dk. Edwin Mhede alisema “Tumeendelea kudhihirisha
ufanisi na ustahimilivu mkubwa kwenye biashara. Tutaendelea kujumuisha
mafanikio makubwa yaliyopatikana, tuendelee kuzingatia kuwainua
wafanyakazi wenye ujuzi unaofaa ili kuwasaidia kufanya kazi kwa ufanisi.
Ninawahakikishia wanahisa wote wa Benki ya NMB, dhamira ya Bodi ni
kufanya maamuzi sahihi ya kifedha na kuongeza faida kwa wanahisa wetu
kwa miaka mingi ijayo”.
No comments:
Post a Comment