HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, May 31, 2022

Washindi wa Tano Bora Miss Tanzania 2022 wakabidhiwa zawadi

Mkurugenzi wa Wateja Wadogo na Wakati wa Benki ya CRDB, Boma Labala, akimkabidhi zawadi mshindi wa Miss Tanzania 2022, Halima Kopwe, katika hafla iliyofanyika Makao Makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam leo. Benki ya CRDB imeungana na waandaji na wadhamini kwa kutoa zawadi mbalimbali zikiwemo fedha taslimu Sh. Mil. 5, Bima ya Maisha yenye thamani ya Sh. Mil. 50 na bima kubwa ya gari, pamoja na bima ya safari. Kushoto ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Startimes, Luo Hao na kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa benki hiyo, Stephen Adili.
Mkurugenzi wa Wateja Wadogo na Wakati wa Benki ya CRDB, Boma Labala (wa pili kulia), Afisa Mtendaji Mkuu wa Startimes, Luo Hao (wa pili kushoto), Meneja Masoko wa Strategis, Lilian Suka (kulia) kwa pamoja wakimkabidhi mfano wa zawadi ya bima ya Safari za Miss Tanzania 2022, Halima Kopwe, za nje ya nchi. Kushoto ni mwakilishi kutoka Basata, hafla hiyo ilifanyika Makao Makuu ya benki ya CRDB jijini Dar es Salaam leo.


========   ========   =========

Waandaji wa shindano la Miss Tanzania kampuni ya ‘The Look’ kwa kushirikiana na wadhamini wa shindano hilo Startimes, Benki ya CRDB, na kampuni za bima za Sanlam na Strategis, wamekabidhi zawadi kwa walimbwende walioingia katika tano bora katika kinyang’anyiro cha Miss Tanzania 2022 ambapo mlimbwende Halima Kopwe kutoka Mtwara aliibuka kidedea, Mashindano hayo yalifikia kilele mnamo Tarehe 20 Mwezi Mei 2022. 
Akizungumza katika hafla ya kukabidhi zawadi iliyofanyika Makao Makuu ya Benki ya CRDB yaliyopo barabara ya Ali Hassan Mwinyi Jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa kamati ya Miss Tanzania Azama Mashango alisema zawadi, hizo ni sehemu ya ahadi ambazo zilitolewa kwa washiriki wa shindano hilo, huku akiwashukuru wadhamini wote waliojitokeza kufanikisha Miss Tanzania 2022.

“Leo hapa tunakabidhi zawadi kwa walimbwende walioingia katika tano bora kama ambavyo taratibu za mashindano zinavyojieleza. Zawadi zitakazokabidhiwa ni pamoja na bima ya maisha yenye jumla ya thamani ya Shilingi Milioni 50 kwa muda wa miaka mitano kutoka kampuni ya Sanlam life, bima ya gari kwa mshindi wa kwanza kwa ajili ya kukinga na majanga yatokananyo na ajali,kutoka sanlam general, bima ya safari kwa safari zote za mashindano ya nje kwa mwaka mzima kutoka kampuni ya strategies , na zawadi za fedha taslimu,” alibainisha Azama.
Akikabidhi zawadi ya bima ya gari kwa mshindi wa kwanza wa Miss Tanzania 2022, Mkuu wa Kitengo cha Bima Benki ya CRDB, Moreen Majaliwa alisema zawadi hiyo itamsaidia kumkinga mshindi huyo ambaye alipewa zawadi ya gari aina ya benz katika majanga yanayosababishwa na ajali. 

“Thamani ya gari aliyopewa mrembo wetu Halima ni Shilingi Milioni 30, ni gari ya thamani kubwa, hivyo inapaswa kuwekewa ulinzi wa kibima ili aweze kufurahia matunda ya shindano hili. Benki yetu kupitia kitengo cha bima tumesema tutamsaidia kufanikisha hili kwa kumkatia bima ya mwaka mzima ili kumkinga na majanga,” alisema Moreen.

Moureen alisema kuwa kwa kutambua mchango wa mashindano hayo katika kuwainua vijana wakike na kulitangaza Taifa, Benki hiyo kwa kushirikiana na washirika wake wa kampuni za bima za Sanlam na Strategis pia wametoa bima ya maisha zenye jumla ya Shilingi Milioni 50, pamoja na bima ya safari ya mwaka kwa walimbwende ambao watashiriki mashindano ya kimataifa.

“Shindano la Miss Tanzania limekuwa daraja la mafanikio kwa vijana wengi wa kike wenye sifa za urembo. Lakini pia limesaidia kubadilisha mtazamo wa jamii juu ya kujishughulisha na maswala ya urembo. Sasa hivi wengi wetu tunatazama Sanaa ya Urembo kama ajira kwasababu ya mafanikio ambayo yanatokana na shindano hili dunia kote,” aliongezea Moureen.

Pamoja na zawadi hizo, Benki ya CRDB pia iliwafungulia washindi hao akaunti na kuwawezesha kupokea zawadi zao za fedha ambapo mshindi wa kwanza alikabidhiwa kiasi cha shilingi milioni 10,  mshindi wa pili shilingi milioni 5, mshindi wa tatu shillingi milioni 3, mshindi wa nne shillingi milioni 1, na mshindi wa tano shilingi milioni 1. Benki hiyo pia iliahidi kutoa elimu ya fedha bure ilikuwasaidia kufikia malengo yao ya kifedha.

Akizungumza kwaniba ya walimbwende hao baada ya kukabidhiwa zawadi mshindi wa taji la Miss Tanzania 2022, Halima Kopwe alitoa shukrani za dhati kwa waandaaji wa shindano hilo, pamoja na wadhamini kwa zawadi hizo. “Zawadi hizi zinaonyesha ni kwa namna gani mashindano ya urembo yameanza kupewa heshima na wadau mbalimbali. Hii itasaidia kuwavutia wasichana wengi ambao wana ndoto ya kushiriki na kukuza ajira katika eneo la urembo,” alisema.
 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad