HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, May 8, 2022

TIC yawavuta wawekeza kutoka Jamhuri ya Czech

 

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC),Dkt. Maduhu Kazi(kushoto) akizungumza jambo na Balozi wa Jamhuri ya Czech nchini kenya na Tanzania Martin Klepetko(katikati) muda mfupi baada ya mazungumzo yaliyofanyika ofisini kwake Jijini Dar es salaam walipotembelea na kufahamu fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo nchini. kulia ni Balozi Miloslav Machalek.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC),Dkt. Maduhu Kazi(kushoto) akizungumza kwenye kikao na Mabalozi kutoka Jamhuri ya Czech Balozi Miloslav Machalek(kulia) na Balozi Martin Klepetko(wapili kulia) mara baada ya mabalozi hao kutembelea ofisi za TIC kwa lengo la kupata maelezo ya fursa za uwekezaji zilizopo nchini.

Na Mwandishi Wetu Dar es Salaam
KATIKA kuhakikisha inaunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kuitangaza Tanzania kupitia sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya uwekezaji, Kituo Cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kimewaalika wawekezaji kutoka Jamhuri ya Czech kuja kuwekeza nchini hasa katika sekta za kilimo, Uvuvi na Utalii.

Akizungumza mara baada ya kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Czech Bw Martin Klepetko aliyeambatana na Balozi kutoka Idara ya Diplomasia ya Uchumi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje Czech Bw. Miloslav Machalek, Mkurugenzi Mtendaji TIC, Dkt. Maduhu Kazi mbali ya kuwapatia taarifa mbalimbali za uwekezaji nchini, amesema Tanzania kwa sasa imekua sehemu maridhawa kutokana na uwepo wa rasilimali nyingi ambazo ni lulu kwa taifa.

“Kwanza nichukue fursa hii kuwapongeza kwa ujio wenu nah ii inatupa picha sisi kama wadau namba moja wa uwekezaji nchini kuwa kuna kazi kubwa inafanywa na sio kwetu tu bali hata na Rais wetu ambaye amekuwa mstari wa mbele kuitangaza nchi”, Alisema Dkt. Maduhu.

Dkt Maduhu aliongeza kuwa, kutoka mwezi januari mpaka machi mwaka huu idadi ya wawekezaji 189 walikuja nchini kuangazia fursa zilizopo huku sehemu kubwa ya watu kutoka Jamhuri ya Czech wamevutiwa zaidi kuwekeza kwenye sekta ya Utalii.

“Kwa mujibu wa Balozi hapa ananiambia kumekuwa na ushawishi mkubwa kwao kuja kuwekeza kwenye sekta ya utalii na ushahidi mzuri ni pale ambapo kwa sasa baadhi ya wawekezaji hao wamejenga sehemu za mapumziko hasa Zanzibar”.

Kwa upande wake Balozi Martin Klepetko amesema Tanzania ni nchi yenye fursa nyingi ambazo zikiendelezwa na kutumiwa vyema manufaa makubwa yatapatikana na kusisitiza kuwa sekta ya uwekezaji ni sekta nyeti yenye kutengeneza ajira nyingi duniani.

“Ni faraja kubwa kwetu sisi kuwa hapa, tumejifunza mengi kupitia mazungumzo yetu, sekta hii ya uwekezaji ni pana lakini niwahakikishie kuwa ni sekta ambayo kwa kiasi kikubwa inapunguza changamoto ya ajira ikisimamiwa vyema”, Alisema Bw Klepetko.

Aidha Bw. Klepetko aliongeza kuwa,“Kupitia mazungumzo haya na sisi tutakuwa mabalozi wakutangaza fursa adhimu zilizopo hapa ili watu wa Czech waje kuwekeza Tanzania”.

Naye Bw. Miloslav Machalek amesema maendeleo ya uchumi wa taifa lolote lile duniani yanategemea uwekezaji huku akibainisha kuwa sekta ya utalii ni miongoni mwa sekta inayowavuta wa Czech wengi zaidi kuja Tanzania.

“Unapozungumzia uwekezaji unagusa moja kwa moja uchumi kwa kuwa sekta hizi zina uhusiano mkubwa sana kwa maendeleo ya taifa”.

Matarajio ya TIC ni kuona wawekezaji wengi wanakuja nchini ikiwa na matunda pia yanayotokana na jitihada endelevu zinazofanywa na serikali.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad