HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, May 13, 2022

RAIS DK.MWINYI KUFUNGUA WIKI YA MAKISATU JIJINI DODOMA

 


Na Janeth Bocco-DODOMA
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Wiki ya Ubunifu ya mwaka 2022.

Maadhimisho hayo ambayo yanakwenda sambamba na Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) ambayo yanatarajia kuanza Mei 15 hadi Mei 20,2022 jijini Dodoma

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Mei 12,2022 Jijini Dodoma,Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia Prof.Adolf Mkenda,amesema kuwa Rais Mwinyi atazindua rasmi maadhimisho hayo Mei 16 katika uwanja wa Jamhuri.

Pia, amesema Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk .Philip Mpango anatarajiwa kufunga maadhimisho hayo Mei 19 mwaka huu.

Waziri Mkenda amesema kuwa mashindano hayo yataibua, kutambua, kuadhimisha, kujenga, kukuza na kuendeleza ubunifu wa Watanzania katika nyanja za Sayansi na Teknolojia ili kuchangia juhudi za maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Hata hivyo, bunifu 862 zimesajiliwa kwa ajili ya Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU 2022).

Waliosajiliwa ni kutoka makundi ya Shule za Msingi ni bunifu 38 na Shule za Sekondari ni bunifu 273, Vyuo vya Ufundi Stadi (36), Vyuo vya Kati (124), VyuoVikuu (127), Taasisi za Utafiti na Maendeleo(30) na Mfumo usio Rasmi(234).

Prof.amesema kuwa mbali na fainali za MAKISATU kutakuwa na maonesho mbalimbali ya bunifu na teknolojia za wabunifu wa Kitanzania, maonesho ya huduma na bidhaa zinazotolewa na taasisi mbalimbali nchini.

“Maonesho yanatoa fursa kwa wabunifu au wagunduzi kujitangaza na kujulikana kwa wawekezaji, watumiaji wa bidhaa zao na wadau wengine wa ndani na nje ya nchi.

Amesema kuwa maadhimisho ya wiki ya MAKISATU ni sehemu ya mikakati ya Serikali ya awamu ya sita ya kuongeza hamasa ya matumizi ya sayansi na kwamba maadhimisho hayo yatafanyika katika ngazi ya Mikoa na Taifa.

“Mikoa iliyofanikiwa kuandaa maadhimisho ya wiki ya ubunifu kwa mwaka huu ni pamoja na Dar es Salaam,Dodoma,Mbeya,Arusha,Iringa,Mwanza,Zanzibar,Tanga,Kilimanjaro,Morogoro,Njombe,Kagera,Mtwara,Kigoma,Mara na Ruvuma,”amesema.

Waziri Mkenda amesema katika ngazi ya mikoa maadhimisho haya yanaratibiwa kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia,COSTECH na programu ya FUNGUO chini ya Shirika la UNDP.

“Kupitia kumbi za ubunifu,vituo vya ubunifu,taasisi za umma na binafsi Katika mikoa husika ambapo uratibu huu inahusisha Ofisi ya Rais-TAMISEMI kupitia maafisa maendeleo ya jamii.

“Katika ngazi zote mbili,mikoa na Taifa, MAKISATU yataambatana na matukio mbalimbali ikiwa ni pamoja na kilele chake yatakayolenga kupata washindi kwa mwaka 2022.

Amesema washindi hao ni katika ngazi ya kitaifa,majukwaa ya majadiliano kuhusu maendeleo ya Sayansi, Teknolojia na ubunifu nchini yanayohusisha utafiti na ubunifu.

Vilevile, amesema katika maadhimisho hayo kutakuwa na mafunzo na semina kwa wabunifu ikiwemo elimu na ujasiriamali.

“Nitumie nafasi hii kuwataka wabunifu na wananchi wote kushiriki katika maadhimisho hayo na kuendelea kutumia bunifu mbalimbali zinazotokana na watanzania katika shughuli za maendeleo,”amesema

Kaulimbiu Wiki ya Ubunifu kwa mwaka 2022 ni “Ubunifu kwa Maendeleo Endelevu”.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad