HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, November 3, 2021

TANZANIA YAPIGA HATUA KUBWA MABORESHO SEKTA YA AFYA - Prof. Makubi

 


Na.WAMJW-Dodoma
KATIBU Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Abel Makubi amesema, Tanzania inazidi kupiga hatua katika maboresho ya Sekta ya Afya kulingana na tathmini iliyofanywa kutoka mwaka 2015 hadi mwaka 2020.

Prof. Makubi, amesema hayo mapema leo Novemba, 03, 2021 wakati wa Mkutano wa 22 wa kitaalam wa kutathmini utekelezaji wa vipaumbele vya sekta ya afya kwa mwaka 2020/21. Jijini Dodoma.

Prof. Makubi amesema kutokana na mikakati na afua mbalimbali zilizotekelezwa, Tanzania imepata matokeo chanya huku akitolea mfano utoaji wa Huduma za akina mama kujifungulia kwenye vituo vya kutolea huduma za afya zimeongezeka kutoka asilimia 50 mwaka 2015 hadi asilimia 83.1 mwaka 2020 ambayo ni zaidi ya lengo la Mpango Mkakati wa Nne wa Sekta ya Afya (HSSP IV) ambao ni asilimia 65. Iliyokuwa imelengwa hapo awali.

“Nchi vilevile imepiga hatua katika kudhibiti VVU/UKIMWI, Kifua Kikuu, Malaria, Kuhara na magonjwa ya Watoto, aidha katika suala la VVU/UKIMWI, utekelezaji wa 90 90 90 ambapo kwenye viashiria vya upatikanaji wa dawa za kufubaza VVU umeongezeka kutoka asilimia 62 2015 (90 ya kwanza) mwaka 2015 hadi asilimia 84 mwaka 2020 na 90 ya tatu umeongezeka kutoka asilimia 87 kwa mwaka 2015 hadi asilimia 95 mwaka 2020. Amesema Prof. Makubi na kuongeza kuwa, Wanawake wenye VVU wanaotumia dawa za kufubaza virusi kwa ajili kuzuia Maambukizi ya Mama kwenda kwa Mtoto pia imeimarika kutoka asilimia 65 mwaka 2015 hadi asilimia 97.7 mwaka 2020.

Katibu Mkuu Makubi ameongeza kuwa, kiwango cha utambuzi na kutoa matibabu ya aina zote za Kifua Kikuu (Treatment Coverage) kimeongezeka kutoka asilimia 36 mwaka 2015 hadi asilimia 64 mwaka 2020.

Kwa upande wa Malaria Prof. Makubi amesema mahudhurio ya nje kwa wagonjwa wa Malaria yameendelea kupungua kutoka 122 mwaka 2015 kwa kila watu 1,000 kwa mwaka hadi kufikia 106 kwa mwaka 2020 kwa kila watu 1,000.

Katika hatua nyingine Katibu Mkuu Makubi, amezungumzia kuhusu UVIKO-19 ambapo amesema kulingana na mada ya mkutano huu iliyojikita kwenye Ustahimilivu wa Mfumo wa Afya Katika Muktadha wa UVIKO-19: Kujenga dhana ya tuliyojifunza kutokana na Janga hili. Amesema, UVIKO-19 umesababisha athari kubwa ikiwa ni pamoja na watu kupoteza maisha na kuweka athari mifumo ya afya ya jamii katika hali ya sintofahamu.

Prof. Makubi amesema hadi kufikia Oktoba 19, 2021 jumla ya watu 949,377 walikuwa wamechanjwa chanjo ya Janseen. Hii inatafsiri kuwa asilimia 8 ya walengwa wamepewa chanjo. Aidha, Utolewaji wa Chanjo ya Sinopharm umeanza kutolewa tarehe 12 Oktoba, 2021 ambapo mpaka sasa watu 106,315 wamepokea dozi hiyo ya kwanza ya Sinopharm ambayo ni sawa na asilimia 10 ya chanjo hiyo.

Kuhusiana na suala la Bima ya Afya kwa wote, Prof. Makubi, amesema, takriban asilimia 70 ya watu hawana bima ya aina yoyote hali inayosababisha umaskini kutokana na matumizi makubwa katika huduma za afya hivyo Serikali inakamilisha muswada unaosubiriwa kwa muda mrefu kuhusu Bima ya Afya kwa Wote (UHI) unaotarajiwa kuwasilishwa katika kikao cha Bunge pindi utakapokamilia.“Hii itasaidia Watanzania walio wengi ambao ni masikini kupata huduma za Afya. Hivyo, Serikali inatarajia msaada wenu wakati wa utekelezaji wake”.

Awali akitoa salaama za Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali, Dkt. Grace Magembe, alisema Wizara hizo mbili zimekuwa na ushirikiano wa karibu katika kuongoza sekta ya afya hapa nchini kwa kushirikiana na wadau wengine katika kuisukuma sekta hiyo muhimu.

Dkt. Magembe, amesema TAMISEMI, ambayo imekuwa Msimamizi wa maelekezo kutokana na Miongozo ya Wizara ya Afya, wameweza kufanikiwa katika maeneo tofauti, ikiwepo wakati wa sasa wanapoendelea na ujenzi wa Hospitali za Wilaya 20 kwenye Wilaya ambazo hazikuwa na Hospitali.

Dkt. Magembe, alitumia fursa hiyo, kuwapongeza Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Viongozi wa Dini na wale wa Kimila kwa jinsi walivyokuwa mstari wa mbele, kwenye Mpango Harakishi na Shirikishi wa jamii awamu ya kwanza, ulivyosimamiwa na Wizara hizo mbili katika Mapambano dhidi ya Uviko-19 na Mpango wa afua ya chanjo ya Uviko-19.

Mkutano wa 22 wa kitaalam wa kutathmini, utekelezaji wa vipaumbele vya sekta ya afya kwa mwaka 2020/21 unafanyika jijini Dodoma na kuhudhuriwa na wadau wa afya kutoka Serikalini, asasi za kiraiya pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo.
 Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii JInsia, Wazee na Watoto, Prof. Abel Makubi akifungua Mkutano wa 22 wa kitaalam wa kutathmini utekelezaji wa vipaumbele vya Afya.
Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, wakiongoza wajumbe, kwenye uzinduzi wa mpango wa pili Shirikishi na Harakishi wa Mapambano ya Uviko -19 kwakutumia afua ya Chanjo jijini Dodoma wakati wa Mkutano huo.Washiriki wa Mkutano huo, walipokuwa wakifatilia kwa karibu wakati wa ufunguzi wa Mkutano huo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad