HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, October 28, 2021

TMA YATABIRI MVUA CHACHE, YASHAURI TAHADHARI KUCHUKULIWA

 

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dk. Agnes Kijazi akizungumza na waandishi wakati wa utabiri wa muelekeo wa mvua za msimu mwezi Novemba 2021 hadi Aprili 2022, leo Oktoba 27,2021 jijini Dar es Salaam. Kulia kwake ni Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri Mamlaka ya Hali ya Hewa TMA, Dkt. Hamza Kabelwa.
 
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dk. Agnes Kijazi akizungumza na waandishi wakati wa utabiri wa muelekeo wa mvua za msimu mwezi Novemba 2021 hadi Aprili 2022, leo Oktoba 27,2021 jijini Dar es Salaam.

MAMLAKA ya Hali ya hewa Tanzania (TMA) imesema Upungufu wa Mvua unatarajiwa kujitokeza kwa maeneo yanayopata msimu mmoja wa Mvua kwa mwaka unaoanza mwezi Novemba 2021 hadi Aprili 2022.

Imeelezwa kuwa mvua hizo zinatarajiwa kuwa chache yaani za chini ya wastani hadi wastani katika maeneo mengi ya mikoa ya kigoma, Tabora, Katavi, Singida, Dodoma, Rukwa, Songwe, Mbeya na Iringa huku kwa mikoa ya Njombe, Ruvuma, Lindi, Mtwara na kusini mwa mkoa wa Morogoro mvua zikitarajiwa kuwa wastani hadi chini ya wastani.

Mkurugenzi wa TMA, Dkt Agnes Kijazi ameyasema hayo leo Oktoba 27, 2021 jijini Dar es salaam wakati akitoa utabiri wa hali ya hewa kwa waandishi wa habari.

Amesema kuwa vipindi virefu vya ukavu vinatarajiwa kuwa kati ya mwezi Novemba 2021, na Januari 2022 huku Ongezeko la kidogo la mvua likitarajiwa Machi 2022.

Amesema kuwa Mvua katika maeneo mengi  zinatarajiwa kuanza kunyesha katika wiki ya tatu ya mwezi Novemba 2021, na kuisha kati ya wiki ya pili na ya tatu ya mwezi Aprili 2022.

Kufuatia hali hiyo ya mvua chache Dkt Kijazi amezitaja athari zinazoweza kujitokeza ni pamoja na upungufu wa unyevunyevu katika udongo unatarajiwa kujitokeza katika maeneo mengi yanayopata mvua za msimu na kuathiri ukuaji wa mazao.

Aidha Mkurugenzi huyo amesema kina cha maji katika mito mabwawa na hifadhi za maji ardhini kinatarajiwa kupungua hususani katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za chini ya wastani huku mlipuko wa Magonjwa ukitarajiwa kujitokeza kutokana na upungufu wa upatikanaji wa maji safi na salama.

Amesema Mwelekeo huo unaonesha kuchangiwa na Joto la Bahari Katika Vyanzo hivyo Vya Mvua kwa nchi ya Tanzania kuwa la Wastani.

Pia ushauri na tahadhari zimetolewa kwa wadau wa sekta mbalimbali wanaotumia taarifa za hali ya hewa katika utekelezaji wa majukumu yao kama vile kilimo na usalama wa chakula, mifugo na uvuvi, maliasili, wanyamapori na utalii, nishati na maji, usafirishaji (nchi kavu, kwenye maji na angani), mamlaka za miji, afya, sekta binafsi pamoja na menejimenti za maafa.

Mvua za Msimu ni mahususi katika maeneo ya magharibi mwa nchi, kanda ya kati, nyanda za  juu kusini magharibi, kusini mwa nchi, ukanda wa pwani ya kusini pamoja na maeneo ya kusini  mwa mkoa wa Morogoro. Maeneo haya yanapata msimu mmoja wa mvua kwa mwaka, unaoanza mwezi Novemba na kuisha kati ya mwezi Aprili na Mei ya mwaka unaofuata. 

Kutokana na mifumo ya hali ya hewa inayotarajiwa mvua za chini ya wastani hadi wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya mikoa ya Kigoma, Tabora, Katavi, Singida, Dodoma, Rukwa, Songwe, Mbeya na Iringa. Aidha,  mvua za wastani hadi chini ya wastani zinatarajiwa katika baadhi ya maeneo ya mikoa ya  Njombe, Ruvuma, Lindi, Mtwara na kusini mwa Morogoro.

Katika nusu ya kwanza ya msimu  (Novemba - Januari) vipindi virefu vya ukavu vinatarajiwa. Hata hivyo, ongezeko kidogo la  mvua linatarajiwa mwezi Machi, 2022 katika nusu ya pili ya msimu.

Mvua za chini ya wastani hadi wastani zinatarajiwa katika mikoa ya Kigoma, Tabora na Katavi. Mvua hizo zinatarajiwa kuanza katika wiki ya tatu ya mwezi Novemba, 2021 katika  maeneo mengi. Mvua hizo zinatarajiwa kuisha wiki ya pili ya mwezi Aprili, 2022 katika mkoa  wa Katavi na wiki ya tatu ya mwezi Aprili, 2022 katika maeneo mengine yaliyosalia. 

Mvua katika maeneo haya zinatarajiwa kuwa za chini ya wastani hadi wastani na  zinatarajiwa kuanza kati ya wiki ya pili na ya tatu ya mwezi Disemba, 2021. Mvua  zinatarajiwa kuisha wiki ya tatu ya mwezi Aprili, 2022. Nyanda za juu kusini magharibi (Mikoa ya Rukwa, Songwe, Mbeya, Iringa, Njombe,  pamoja na maeneo ya kusini mwa mkoa wa Morogoro):

Mvua za chini ya wastani hadi wastani zinatarajiwa katika maeneo ya mikoa ya Rukwa, Iringa, Songwe na Mbeya.

Aidha, mvua za wastani hadi chini ya wastani zinatarajiwa katika mikoa ya Njombe, kusini mwa Morogoro na maeneo ya miinuko ya mkoa wa Mbeya. Mvua  katika maeneo haya zinatarajiwa kuanza kati ya wiki ya tatu na ya nne ya mwezi Novemba, 2021 na kuisha katika wiki ya tatu ya mwezi Aprili, 2022. Hata hivyo, maeneo ya kusini mwa mkoa wa Morogoro mvua zinatarajiwa kuanza wiki ya pili ya mwezi Novemba, 2021 na  kuisha wiki ya kwanza ya mwezi Aprili, 2022.

Pwani ya kusini na maeneo ya kusini mwa nchi (Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma): Mvua za wastani hadi chini ya wastani zinatarajiwa katika maeneo ya mikoa ya Lindi,  Mtwara na Ruvuma. Mvua zinatarajiwa kuanza wiki ya pili ya mwezi Novemba, 2021 katika  mikoa ya Lindi na Mtwara na wiki ya tatu ya mwezi Novemba, 2021 katika mkoa wa  Ruvuma. Mvua zinatarajiwa kuisha katika wiki ya nne ya mwezi Machi, 2022 katika mkoa wa Ruvuma na wiki ya pili ya mwezi Aprili, 2022 katika mikoa ya Lindi na Mtwara.

Aidha, upo uwezekano wa kutokea kwa mgandamizo mdogo wa hewa kaskazini mashariki mwa kisiwa cha Madagascar, hivyo kusababisha kurejea kwa mvua katika baadhi ya  maeneo mwishoni mwa mwezi, Aprili, 2022.

TMA inawashauri wakulima kupanda mazao na mbegu zinazokomaa ndani ya muda mfupi na  zinazostahimili mvua chache kama vile mazao jamii ya mizizi na mazao ya bustani huku wakishauriwa kutumia mbinu na teknolojia za kilimo himilivu za kuhifadhi maji na  unyevunyevu wa udongo.  

“Wakulima wazingatie kupata ushauri kutoka kwa maafisa ugani juu  ya namna bora ya kuendesha kilimo kwa usalama wa chakula na lishe huku mamlaka husika zikishauriwa kutoa elimu na ushauri kwa wakulima juu ya njia bora na  namna ya kutumia kiwango kidogo cha mvua kinachotarajiwa pamoja na matumizi mazuri ya  akiba ya chakula kilichopo..

Aidha mamlaka imesema sekta za usafirishaji hususan usafiri wa ardhini, anga na kwenye maji zinaweza kunufaika  kutokana na vipindi vya ukavu vinavyoweza kujitokeza.

Hata hivyo, mamlaka ya Hali ya Hewa I imewashauri wadau kuwasiliana na Mamlaka ili kupata taarifa mahsusi za utabiri wa msimu ili  kukidhi mahitaji maalum katika sekta zao.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad