Waziri
wa Ujenzi na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa amesema ataunda timu ya
uchunguzi ili kujiridhisha kama gharama za ujenzi unaoendelea katika
uwanja wa ndege wa Arusha zinawiana na thamani ya fedha.
Profesa
Mbarawa amesema hayo mara baada ya kukagua upanuzi na ukarabati wa
miundombinu ya maegesho ya ndege, magari na njia ya kuruka na kutua
ndege (run way) katika uwanja huo.
“Nimekagua
kazi ni nzuri hongereni, ila nitaleta timu hapa iniambie hizi gharama
za ujenzi mnazozitaja kama zinaendana na thamani ya fedha”, amesema
Prof. Mbarawa.
Amewataka
wafanyakazi wa uwanja wa ndege huo kufahamu umuhimu wao katika kutoa
huduma bora kwa watalii na abiria wengine ili kuvutia watu wengi kutumia
uwanja huo na hivyo kuongeza mapato.
Amesisitiza
kuwa uwanja wa ndege wa Arusha ni wa tatu kwa mapato na wa pili kwa
miruko ya ndege na abiria katika biashara ya usafiri wa anga hapa nchini
ukitanguliwa na uwanja wa ndege wa Dar es Salaam (JNIA) na Mwanza hivyo
Serikali inautazama kikamilifu.
Naye
Kaimu Meneja wa uwanja wa ndege huo Bw, Reston Mtafya amesisitiza kuwa
watumishi wamejipanga vizuri kimaadili, nidhamu na ubunifu ili kuleta
tija katika kazi zao.
“Tumejipanga kuhakikisha uwanja wetu unatumiwa na abiria wengi kwa kutoa huduma za viwango vya juu”, amesisitiza Mtafya.
Katika
hatua nyingine Waziri huyo wa Ujenzi na Uchukuzi amekagua karakana ya
Wakala wa Ufundi na Umeme nchini TEMESA mkoa wa Arusha na kuwataka
kufanyakazi zinazopimika na kumpa ripoti za kazi hizo kila mwezi.
Amewataka
kuhakikisha malalamiko ya watumiaji huduma za TEMESA yanafika mwisho
kwa kutoa huduma za kisasa, kibingwa na za haraka katika fani ya
utengenezaji wa magari, mitambo na umeme .
“Kila
mwezi nataka ripoti ioneshe mezalisha kiasi gani cha fedha, mmekusanya
shilingi ngapi na mmetoa huduma kwa kiwango gani ili tuwapime na
watakaoshindwa watupishe”, amesisitiza Prof. Mbarawa.
Amezungumzia
umuhimu wa TEMESA kufanya majukumu yake ya msingi katika kutoa huduma
na kuwatumia wahitimu wa VETA na Vyuo vya Ufundi kufanya mazoezi ili
kuwajengea uwezo wakati wanatafuta ajira.
Prof. Mbarawa yuko katika ziara ya siku tatu mkoani Arusha kukagua miradi ya maendeleo ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.
No comments:
Post a Comment