Waziri wa Kilimo Mhe Prof. Adolf Mkenda akikagua ujenzi wa maghala na vihenge vya kisasa vya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) wakati alipofanya ziara ya kikazi ya siku moja Wilaya ya Babati Mkoani Manyara leo tarehe 16 Agosti 2021.
Waziri wa Kilimo Mhe Prof. Adolf Mkenda akipata maelezo ya ujenzi wa maghala na vihenge vya kisasa vya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) wakati alipofanya ziara ya kikazi ya siku moja Wilaya ya Babati Mkoani Manyara leo tarehe 16 Agosti 2021.
Waziri wa Kilimo Mhe Prof. Adolf Mkenda akikagua mitambo ya kusafisha nafaka kwenye ujenzi wa maghala na vihenge vya kisasa vya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) wakati alipofanya ziara ya kikazi ya siku moja Wilaya ya Babati Mkoani Manyara leo tarehe 16 Agosti 2021.
Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Manyara
Serikali
imebainisha kuwa kuchelewa kukamilika kwa ujenzi wa Vihenge vya Kisasa
na Maghala kumetokana na tatizo la mgogoro wa mwingiliano wa viwanja
kati ya Shirika la umeme (TANESCO) na Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya
Chakula (NFRA).
Mgogoro
huo ulipelekea mkandarasi kusimama na baadaye kuongezewa muda wa
mkataba wa kutekeleza mradi mpaka tarehe 13 Septemba 2021.
Akizungumza
mara baada ya kufanya ziara ya kikazi ya siku moja Wilaya ya Babati
Mkoani Manyara leo tarehe 16 Agosti 2021 Waziri wa Kilimo Mhe. Prof.
Adolf Mkenda amesema kuwa pamoja na mradi huo kukamilika kwa asilimia
99.8 kama inavyotajwa lakini bado NFRA inapaswa kuzifanyia kazi
changamoto mbalimbali kabla ya kukabidhiwa mradi huo.
Waziri
Mkenda amebainisha kuwa changamoto hizo ni pamoja na kupewa elimu ya
namna gani vihenge hivyo vitaweza kufanyiwa usafi kwani kwa sasa hakuna
uwezekano wa kufanya usafi jambo ambalo ni hatari kwa uhifadhi wa nafaka
zinazonunuliwa na kuhifadhiwa na serikali.
Pia
ameitaka NFRA kuhakikisha kuwa inasimamia utekelezaji wa uwezekano wa
njia sahihi ya kutibu nafaka inayohifadhiwa kwenye Vihenge hivyo vya
kisasa (Fumigation) kwani eneo hilo ni muhimu zaidi kwa ajili ya
uhifadhi.
Ujenzi
wa Vihenge vya Kisasa na Maghala kanda ya Arusha inayojumuisha mikoa ya
Arusha na Manyara katika kituo cha Babati unatekelezwa na kampuni ya
Unia Sp.zo.o kutoka nchini Poland kwa kushirikiana na kampuni ya wazawa
ya Elerai Construction Company Ltd kwa gharama ya Dola za Kimarekani
Milioni 8.08 ambazo ni sawa na Bilioni 18.67 za kitanzania.
Kwa ujumla sehemu kubwa ya mradi imechukuliwa na ujenzi wa vihenge ambao ni zaidi ya asilimia 60 ya mkataba.
Wakala
wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) kwa sasa una maghala 34 yenye
uwezo wa kuhifadhi nafaka Tani 251,000 katika kanda zake nane za
kimakakati.
Hivyo serikali inaendelea na utekelezaji wa mradi huo ambao ni maalumu kwa ajili ya kuongeza uwezo wa kuhifadhi kwa jumla ya Tani 250,000 wenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 55 ambazo ni sawa na Bilioni 126.5 ambapo mradi huo utakapokamilika utaongeza uwezo wa kuhifadhi wa NFRA kutoka Tani 251,000 za sasa hadi kufikia Tani 501,000.
No comments:
Post a Comment