HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, June 21, 2021

HALMASHAURI YA NYASA YATOA MIKOPO YA ASILIMIA 100, RC IBUGE APONGEZA

 

 

MKUU wa Mkoa wa Ruvuma Brigedia Jenerali  Wilbert Ibuge, ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa kwa kutoa mikopo kwa asilimia 100  yenye thamani ya ya zaidi ya shilingi milioni 66.6 kwa  makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

RC Ibuge ametoa pongezi hizo mwishoni mwa wiki katika mkutano maalum wa Baraza la madiwani la Halmashauri hiyo wa kujadili taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali CAG kwa mwaka 2019/2020.

Mkutano huo umefanyika katika Ukumbi wa Kepteni John Komba mjini  Mbambabay Makao makuu ya Wilaya ya Nyasa.

Brigedia Jenerali Ibuge amepongeza mara ya kwanza Halmashauri hiyo kutoa mikopo kwa asilimia 100 ambapo kati ya fedha zilizotolewa Wanawake wamepata milioni 37.6 vijana, milioni 19,000,000 kundi la watu wenye ulemavu shilingi milioni 10,000,000.

Katika hatua nyingine RC Ibuge ameipongeza Halmashauri hiyo kwa kufanikiwa kukusanya mapato ya ndani ya zaidi ya shilingi bilioni 1.2 ambayo ni sawa na  asilimia 82.95.

“Kwa moyo wa dhati kabisa naipongeza Halmashauri  hii kwa kutoa mikopo kwa makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa kuwa makundi hayo ni muhimu katika Uzalishaji mali”,alisisitiza RC Ibuge.

Hata hivyo Mkuu wa Mkoa amewaagiza Madiwani na watendaji wa Halmashauri kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuweza kuinua makusanyo na kutekeleza miradi ya maendeleo kwa asilimia 100.

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa Mhe.Stewart Nombo ameahidi kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Mkuu wa Mkoa kwa maslahi ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad