Na Muhidin Amri,Madaba
MKURUGENZI wa Halmashauri ya wilaya Madaba mkoani Ruvuma Shafi Mpenda
amesema, ujenzi wa jengo la utawala kwa ajili ya watumishi wa
Halmashauri hiyo hadi sasa limekamilika kwa asilimia 99.
Mpenda amesema hayo jana wakati akizungumza na Habarileo ofisini kwake
na kumshukuru Rais Dkt John Magufuli kwa kutoa kiasi cha shilingi
bilioni 3 kwa ajili ujenzi wa jengo hilo ambalo kwa sasa limesaidia
sana watumishi wa idara mbalimbali kutekeleza majukumu yao kwa weledi na
ufanisi mkubwa.
Alisema,walipokea fedha za mradi kwa mafungo ambapo mwaka 2016
walipokea shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga msingi na nguzo za
kusimamisha kuta za jengo.
Mpenda alibainisha kuwa,ujenzi rasmi ulianza Mwezi Septemba 2017 baada
ya kusaini mkataba na wakala wa majengo Tanzania(TBA) wa shilingi
milioni 493 na shilingi milioni 7 zilitumika kwa ajili ya kufanya vipimo
vya udongo kwenye eneo la mradi.
Alisema, Halmashauri kupitia mapato yake ya ndani ilihusika kulipa
fidia ya shilingi milioni 6.78 kwa wananchi waliokuwa wamiliki halali wa
eneo lililotumika kujenga jengo.
Hata hivyo, Serikali iliendelea kutoa fedha na kufikiwa kiasi cha
shilingi bilioni 3 ambazo mpaka sasa Halmashauri imeshazipokea na
kutumia shilingi bilioni 2.9 na kubakiwa milioni 85.
Aidha alisema, Mwezi Mei 2020 Halmashauri ililazimika kuvunja mkataba na
Tba kutokana na changamoto zilizojitokeza ikiwemo kusua sua kwa ujenzi
wa mradi huo ambapo TBA ilijenga Boma tu, hivyo Halmashauri iliomba
kibali Tamisemi kwa ajili ya kumalizia ujenzi kwa kutumia mafundi wa
ndani(force account)kwa kuamini kwamba utaratibu huo utasaidia
kukamilisha mradi.
Kwa mujibu wa Mpenda,baada ya kuomba kibali cha Katibu Mkuu Tamisemi na
Halmashauri iliendelea kujenga jengo hilo kwa mfumo wa force Akaunti
ambao kimsingi umefanikisha kumaliza jengo hilo haraka na idara zote
zimeshahamia.
Alisema,walilazimika kuhamia mapema hasa baada ya kupokea watumishi
wengi na jengo walililokuwa wanalitumia ni dogo,na hata usalama wa
nyaraka za serikali na usalama wa watumishi ulikuwa mdogo hivyo
kushindwa kutekeleza baadhi ya majukumu.
Alisema, ni faraja kubwa kuona sasa watumishi wanachapa kazi ya
kuwahudumia wananchi wa jimbo la Madaba na maeneo mengine ya nchi
licha ya kutokamilika kwa asilimia 100 ambapo kazi ndogo ndogo
zilizobaki zinafanyika wakati wakitumishi wakiwa katika jengo hilo na
kazi zilizobaki ni kufunga milango, na marekebisho kwa maeneo ya nje
kabla ya fundi kurudia kupaka rangi ya mwisho.
Alisema, fedha zilizobaki wameamua kujenga kibanda cha mlinzi aweze
kufanya kazi katika mazingira mazuri,kujenga kantini ili kuwasaidia
watumishi kupata huduma ya chakula karibu na kuokoa muda wa kazi wa
mwajiri ili watumishi wasipate sababu ya kwenda umbali mrefu na
kuchelewa kurudi kuchapa kazi.
Alisema, kukamilika kwa jengo hilo kunakwenda kuchochea morali ya
watumishi kufanya kazi kama ilivyo dhamira ya serikali ya awamu ya tano
na watumishi kuchochea mahudhurio kazini tofauti na siku za ambapo
jengo lililotumika lilikuwa dogo na kuvunja hali ya uwajibikaji kwa
watumishi.
Pia alisema, sasa kumekuwa na usiri mkubwa kwa watumishi pale
anapotekeleza majukumu yake sambamba na kusaidia mtumishi kuona ufahari
kuitanga vyema Halmashauri na Serikali ya awamu ya tano kwani jengo
hilo lina huduma zote muhimu.
Mpenda alieleza kuwa, jengo hilo limebadilisha taswira na kuongeza
thamani ya eneo hilo na sasa wananchi wanaweza kujenga nyumba kwa ajili
ya kupangisha watumishi watakopenda kuishi karibu na ofisi.
Amewataka wananchi kutumia fursa ya kuwepo kwa jengo hilo kujenga nyumba
za kisasa,kujenga Hoteli,kumbi za sterehe na miradi mingine ya
kuwaingizia kipato kwa sababu Serikali imeshasogeza fursa katika meoneo
yao.
Sehemu ya Jengo la Utawala la Halmashauri ya wilaya Madaba mkoani Ruvuma likiwa limekamilika kwa asilimia 99 na limeanza kutumika kwa watumishi wa Halmashauri hiyo kutekeleza majukumu yao ya kila siku.Jengo hilo limegharimu zaidi ya shilingi bilioni 3 linakusudia kuboresha mazingira ya kufanyia kazi watumishi. Picha na Muhidin Amr
No comments:
Post a Comment