Na Zainab Nyamka, Michuzi Tv
MAHAFALI ya 13 ya Chuo Kishirikishi cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) yafana baada ya wanafunzi 1,685 kuhitimu masomo yao katika fani mbalimbali huku wanawake wakishika nafasi za juu.
Wanafunzi hao wamehitimu masomo yao na kutunukiwa fani mbalimbali na Mkuu wa Chuo hicho Rais Mstaafu Dkt Jakaya Mrisho Kikwete leo Jijini Dar es Salaam.
Katika mahafali hayo wanawake wameonekana kushika nafasi za juu katika masomo yao, huku mhitimu kutoka Kitivo cha Sayansi Mesia Aston Simbeye aliweza Kutunukiwa Cheti chake cha kuhitimu Chuo pamoja na tuzo tano kutoka kwa Mkuu wa Chuo hicho Rais Mstaafu Dkt Jakaya Mrisho Kikwete baada ya kupata GPA 4.9
Akizungumza wakati wa mahafali hayo, Rasi wa Chuo Prof Stephen Maluka amesema jumla ya wanafunzi 1,647 watatunukiwa digrii za awali katika fani mbalimbali, 33 Stashahada ya Uzamili katika Elimu, 3 Digrii ya Umahiri ya Elimu Jamii katika Utawala wa Umma na 2 Digrii ya Umahiri katika Elimu jamii na Ualimu.
Amesema katika mwaka huu, kati ya wahitimu wote wanaume ni 989 sawa na asilimia 58.7 na wanawake ni 696 sawa na asilimia 41.3
"Katika mahafali ya 13, Chuo chetu kinakuwa kimetimiza jumla ya wahitimu 14, 765 waliobobea kwenye fani mbalimbali tangu kuanzishwa kwake,"
Aidha, Prof Maluka amesema toka kuanzishwa kwake wahitimu wamekuwa na mchango mkubwa katika sekta ya elimu na kuzisaidia jamii na serikali kwa ujumla kufikia malengo yake.
Aidha, wahitimu wametakiwa kutumia fani zao kujiajiri na kuacha kusubiri kuajiriwa na serikali bali wawe wepesi kuangali ni wapi ujuzi wao unaweza kutumika kwa ufanisi zaidi hata kama itawabidi kufanya kazi kwa kujitolea.
"Kwa kufanya hivyo, mtajenga kujiamini, ujuzi na mchango wenu utatambuliwa na kuinufaisha jamii, zingatieni maadili na miiko ya jamii yetu kokote mtakakokuwa. Jiepusheni na vitendo vya uvunjifu wa amani, ufisadi, rushwa na ubadhirifu wa rasilimali za Taifa,"
Mahafali hayo pia yaliweza kuhudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Temeke Godwin Gondwe na viongozi wengine.
Mkuu wa Chuo Kishirikishi cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi tuzo Mwanafunzi bora kwa mwaka 2020 Mesia Simbeye baada ya kuibuka kinara na kupata GPA 4.9 wakati wa mahafali ya 13 ya Chuo Kishirikishi cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Wahitimu wa Chuo Kikuu Kishirikishi cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) wakisoma kiapo cha utii baada ua kutunukiwa shahada zao mbalimbali wakati wa mahafali ya 13 ya Chuo Kishirikishi cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam
No comments:
Post a Comment