HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, September 4, 2020

TATIZO LA MAJI SIMANJIRO KUWA HISTORIA-MAJALIWA

 

*Ni baada ya Serikali kujenga mradi mkubwa wa sh Bil. 40

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama wilayani Simanjiro kuwa historia baada ya Serikali kujenga mradi mkubwa wa maji kutoka Mto Ruvu hadi Orkesumet wenye thamani ya sh bilioni 40.

“Mradi huu umefikia asilimia 89 za utekelezaji na unatarajiwa kuanza kufanya kazi mwishoni mwa mwezi huu wa Septemba 2020 au mapema Oktoba 2020. Pia Serikali imetekeleza miradi mingine ya maji ikiwemo ya uchimbaji ya mabwawa ya kunyweshea mifugo ambayo tayari inatoa huduma kwa wananchi.”

Ameyasema hayo leo (Ijumaa, Septemba 4, 2020) alipohutubia mkutano wa kampeni uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Orkesumet wilayani Simanjiro mkoani Manyara wakati akimuombea kura Rais Dkt. John Pombe Magufuli na mgombea ubunge wa Jimbo la Simanjiro, Christopher Ole Sendeka na wagombea udiwani.

Amesema miradi mingine inayotekelezwa katika wilaya hiyo ni pamoja na uchimbaji wa visima virefu vya maji 18 katika maeneo ya Kitwai, Msitu waTembo, Mirerani, Londrekes, Loibosoit, Kityangare Namalulu, Terrat, Olbili, Nadonjukin na Okutu. Ukarabati wa visima 13 umefanyika kikamilifu hatimaye vituo vya kuchotea maji vimefikia 95.

“Ujenzi wa bwawa la Narakauo kwa ajili ya matumizi ya mifugo na wananchi wa vijiji vya karibu yake unaendelea kupitia Wizara ya Mifugo kwa gharama ya sh.  413,865,700 sawa na asilimia 36.”

Waziri Mkuu amesema mradi huo utakuwa mkombozi mkubwa kwa wafugaji wa ukanda wote wa Simanjiro ya juu. Pia Serikali imetumia sh. 412,724,300 kutekeleza mradi wa maji kutoka Nomokon hadi Narakauo ambao pia utasaidia kupunguza uhaba wa maji kwa wafugaji wa Kata nzima ya Loibosiret.


Amesema licha ya utekelezaji wa miradi ya maji pia, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili kuboresha barabara za mjini katika Halmashauri ya wilaya hiyo na zile za makao makuu ya wilaya (Orkesumet) ambazo zinaendelea kuwekewa lami. “WanaSimanjiro endeleeni kukiamini Chama chenu Cha Mapinduzi kwa kuchagua wagombea wote wa CCM ili mpate maendeleo zaidi.”

Akizungumzia kuhusu nishati ya umeme, Mheshimiwa Majaliwa amesema kati ya vijiji 56 vya wilaya ya Simanjiro vijiji 38 tayari vimepata umeme na vijiji 18 visivyokuwa na umeme vitapatiwa nishati hiyo, hivyo amewataka wananchi hao waendelee kuwa na subira na kuiamini Serikali yao.

Amesema Rais Dkt. Magufuli anataka kuona kila nyumba ya Mtanzania inapata umeme tena kwa gharama nafuu na ametenga fedha nyingi zitakazotosheleza kusambaza umeme katika vijiji vyote vikiwemo na wilaya ya Simanjiro. Gharama za kuunganishiwa umeme huo zimepungua kutoka sh 177,000 hadi sh. 27,000.

Waziri Mkuu ameongeza kwa kusema wananchi hawatowajibika tena katika kulipia gharama za nguzo wala fomu za maombi ya kuunganishiwa umeme kwa sababu tayari gharama hizo zote zimeshabebwa na Serikali.

Mheshimiwa Majaliwa ametumia fursa hiyo kuwaomba wakazi wa wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara na Watanzania wote bila kujali itikadi za vyama vyao wamchague Rais Dkt John Pombe Magufuli ili aendeleze kazi ya kuwaletea maendeleo katika maeneo yao ambayo tayari ameshaianza.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad