MKURUGENZI
Mtendaji wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB),
Abdul-Razaq Badru amewataka watumishi wa Ofisi hiyo kufanya kazi kwa
bidi, maarifa na nidhamu kwa wateja wake ili kukidhi matarajio ya utoaji
huduma bora kwa wanafunzi waombaji na warejeshaji wa mikopo ya elimu ya
juu nchini.
Akizungumza (Agosti 18, 2020) Jijini Dar es Salaam wakati wa
ufunguzi wa mafunzo elekezi kwa watumishi wapya waliohamia HESLB katika
kipindi cha miezi sita iliyopita, Badru alisema kila mtumishi ndani ya
HESLB anapaswa kutoa huduma bora kwa wateja kwani ndiyo wajibu wa msingi
wa mtumishi wa umma.
Badru alisema wateja ndio msingi mkuu wa uwepo wa taasisi yoyote ya
umma, hivyo ni wajibu wa watumishi wa HESLB kuhakikisha inawadumia vyema
wateja wote wanaofika katika ofisini hapo, ambapo sehemu kubwa ni
pamoja na wanafunzi waombaji mikopo na waliokuwa wanufaika wa mikopo ya
elimu ya juu.
"Wateja wetu ndio watu wanaotuweka mjini, hawa ndio msingi wa uwepo
wetu, tunapaswa kuwahudumia vyema, tusiwe kikwazo kwa wateja kupata
huduma, tufanye kazi kwa nidhamu katika kutekeleza majukumu katika
maeneo yetu ya kazi.’’ Alisema Badru.
Akifafanua Zaidi, Badru alisema ni wajibu wa watumishi hao wapya
kujituma katika maeneo yao ya kazi na kuwapongeza kuhamia HESLB kwa kuwa
taasisi hiyo inatumia mifumo mbalimbali ya kupima walionao katika
kutimiza wajibu wao kwa mujibu wa utaratibu ikiwemo kutumia Mfumo wa
Wazi wa Mapitio na Tathmini ya Utendaji Kazi (OPRAS).
Aidha Badru aliwaka watumishi wa Ofisi hiyo kutunza rasilimali za
umma ikiwemo vifaa na vitendea kazi vinavyotolewa na Serikali kwa ajili
ya matumizi ya ofisi hiyo na kuongeza kuwa watumishi wote kuendelea
kushirikiana katika usimamizi wa rasilimali hizo ili ziwe na matumizi
endelevu kwa manufaa ya taasisi hiyo.
Kwa upande wake Mkufunzi wa Mafunzo hayo kutoka, Chuo cha Utumishi wa
Umma Tanzania (TPSC), Mariam Muhenga alisema utoaji wa huduma bora kwa
wateja ni moja ya misingi ya kanuni za maadili ya utumishi wa umma,
hivyo ni wajibu wa mtumishi wa HESLB kuhakikisha kuwa anasimamia kanuni
hizo ili kuleta tija katika maeneo ya kazi.
Aliongeza kuwa mtumishi wa umma ni kioo katika jamii, hivyo anapaswa
kuzingatia kuwa mfano wa kutazamwa katika taswira chanya wakati wote
anapokuwa anatekeleza wajibu wake katika kutoa huduma kwa wateja.
No comments:
Post a Comment