HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, August 20, 2020

WATOA HUDUMA NDOGO ZA FEDHA WATOLEWA HOFU KUHUSU UTEKELEZAJI WA SHERIA NA KANUNI ZA HUDUMA NDOGO ZA FEDHA

Na Farida Ramadhani, Morogoro

Serikali imeeleza kuwa utekelezaji wa Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha hauna lengo la kuua biashara ya huduma ndogo za fedha nchini bali unalenga kuendeleza na kuboresha usimamizi na udhibiti wa Sekta Ndogo ya Fedha ili kuwa na Sekta ya Fedha imara katika ukuaji uchumi na kupunguza umaskini.

Haya yameelezwa na Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Charles Mwamwaja wakati wa mafunzo ya Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha kwa baadhi ya watendaji wa Taasisi za Umma,Fedha na program za Serikali yaliyofanyika mjini Morogoro.

Dkt. Mwamwaja alisema kuwa ni vema baadhi ya watu wakaacha upotoshaji ambao unawatia hofu kuhusu Sheria hiyo kwa kuwa utekelezaji wake utasaidia kutatua changamoto mbalimbali zilizoathiri Sekta ya Fedha kwa kuweka miongozo ya usimamizi na utaratibu wa kumlinda mtumiaji wa huduma ndogo za fedha ambao ni takribani asilimia 55.3 ya nguvu kazi ya Taifa.

“Sheria hii imetoa muongozo wa shughuli zinazotakiwa kufanywa na watoa huduma ndogo za fedha, namna ya kuendasha biashara ya huduma hizo pamoja na haki za msingi za watumiaji ili kuwawezesha watumiaji kupata faida ambayo itakuza uchumi wa nchi”, alifafanua Dkt. Mwamwaja.

Wawasilishaji katika mafunzo hayo walitoa maelezo ya kina kuhusu taratibu za usajili na uombaji wa leseni kulingana na daraja husika kwa mujibu wa Sheria na kuwatoa hofu wananchi kuwa taritibu hizo ni rafiki na wananchi wote wanaweza kuzifuata na kutekeleza matakwa ya kisheria. 

Mwanasheria kutoka Ofisi ya Rais TaAMISEMI, Bi. Antelma Mtemahanji ni miongoni mwa wawezeshaji hao ambae ameeleza kuwa Vikundi vya Kijamii vya Huduma Ndogo za Fedha vinatakiwa kusajiliwa katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ambapo vinatakiwa kuwa na fomu ya maombi ya usajili, katiba iliyosainiwa na wanachama wote, muhtasari wa mkutano wa uazishwaji pamoja na barua ya utambulisho kutoka Kata, Mtaa au Kijiji ili viweze kusajiliwa.

Kwa upande wa washiriki wa mafunzo hayo waliipongeza Serikali kwa kutoa mafunzo hayo ambayo kwa kiasi kikubwa yatarahisisha zoezi la usajili na ukataji leseni hususan katika kipindi hiki kidogo kilicho bakia kabla ya muda wa kipindi cha mpito kuisha ifikapo tarehe 31 Oktoba, 2020.

Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, Bi. Beng’i Issa ni miongoni mwa washiriki wa mafunzo hayo ambaya ameeleza kuwa utekelezaji wa Sheria hiyo utarahisisha zoezi la kupata takwimu sahihi ya wananchi hususani wa kwenye vikundi vya kijamii vya huduma ndogo za fedha kwa ajili ya kuviwezesha.

 

Kamishina wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha wa Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Charles Mwamwaja akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo ya Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha kwa watendaji wa Taasisi za Umma, Fedha na Program za Serikali, iliyofanyika mjini Morogoro, kushoto ni Naibu Kamishna wa Idara hiyo Bi. Mameltha Mtagwaba, Kulia ni Afisa Mkuu wa Idara ya Usimamizi wa Sekta Ndogo ya Fedha kutoka BoT, Bw. Deogratius Mnyamani na wapili kulia ni Kamishna Msaidizi wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Dionisia Mjema. 

Mwanasheria wa Serikali kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Nyanzala Nkinga akielezea majukumu ya Waziri wa Fedha kwa mujibu wa Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha wakati mafunzo ya Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha kwa watendaji wa Taasisi za Umma, Fedha na Program za Serikali, yaliyofanyika mjini Morogoro

Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha kwa watendaji wa Taasisi za Umma, Fedha na Program za Serikali, wakifuatilia kwa makini mada mbalimbali zilizowasilishwa wakati wa mafunzo hayo, yaliyofanyika mjini Morogoro.
Mrajirs Msaidizi kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania, Bw. Josephati Kisamalala akielezea Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha kwa Vyama vya Ushirika wa Akiba na Mikopo kwa washiriki wa mafunzo ya Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha kwa watendaji wa Taasisi za Umma, Fedha na Program za Serikali, yaliyofanyika mjini Morogoro.
Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, Bi. Beng’I Issa akifuatilia kwa karibu maelezo ya watoa mada mbalimbali wakati wa mafunzo ya Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha kwa watendaji wa Taasisi za Umma, Fedha na Program za Serikali, yaliyofanyika mjini Morogoro.
Kamishna wa Idara ya Uendelezaji Sekta ya Fedha wa Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Charles Mwamwaja akiwakaribisha wageni katika mafunzo ya Sera, Sheria na Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha kwa watendaji wa Taasisi za Umma, Fedha na Program za Serikali, yaliyofanyika mjini Morogoro kushoto ni Kamishna Msaidizi wa Idara hiyo, Bi. Dionisia Mjema.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad